Mtazamohalisi

Saturday, December 11, 2010

Obama Na Kisa Cha Lipstick

Atumia ushawishi wa Cliton kukubalika

Katika hali isiyo kawaida Rais wa Marekani ,Barack Obama amejikuta katika wakati mgumu mbele ya waandishi wa habari. Tukio hili limetokea leo mara baada ya kikao cha dharura na rais wa zamani wa marekani Bill Cliton.

Kama kawaida ilifika muda wa kuzungumza na waandishi wa habari kuelezea juu ya mazungumzo yao.
Na ndipo likaibuka jibu la Obama kumtaka Bill Cliton kuelezea umuhimu wa kukubaliana na Rais Obama juu ya makubaliano yake na chama cha Republican kuhusu kuendelea kutumia sheria ya upunguzaji wa kodi kwa watu wakipato cha juu iliyotumika wakati wa utawala wa George Bush.

Ila jambo lilochukua picha nzima ni tukio la Rais Obama kumuwacha pekee Bill Cliton kukabiliana na maswali ya waandishi wa habari huku yeye akienda kujumuika na Mkewe. Rais Obama aliomba dharura kwa Bill Cliton kwa kumwambia aendelea kwani mkewe Michelle Obama  alikuwa akimsubiri muda mrefu na anachelea kumkwaza.


Swali ambalo wengi wanajiuliza vipi Obama amuwachie Bill Cliton kuendelea kujibu maswali ya waandishi wa habari katika hali ngumu kama hii.Wachambuzi wamekifananisha kitendo hicho na kisa cha lipstick.
Inasemekana  ilitokea mwaka 1961 wakati Muigizaji wa Filamu Eddie Fisher alipomruhusu mkewe  Elizabeth Tailor kwenda Rome akijumuika na muigizaji mwenzie Richard Burton kwenda kuigiza katika filamu gonga hapa Cleopatra  hali yeye akibaki Los Angeles.

Hatimaye mapinduzi ya mapenzi yakaibuka,kwani kitendo cha Fisher kubaki Los Angeles kilimkutanisha na muigizaji wakike wa TV ya Ernie Kovac,Sue Kennedy .Na huko Rome Elizabeth Taylor alifungua ukurasa mpya wa mahusiano wa mapenzi na Richard Burton.

Nini kiliutambulisha ulimwengu juu ya mapinduzi haya ya mapenzi ni kitendo cha Sue Kennedy kuchukua Lipstick nyumbani kwa Elizabeth Taylor na Richard Burton na kumpa rafiki yake wa karibu na hapo ndiyo kosa kwani rafiki yake aliitoa siri kwa shangazi yake ambaye ni mwandishi.

Hatimaye talaka zikatembea na uhusiano mpya wa ndoa ukachanua baina ya Elizabeth Taylor na Richard Burton nahuku Eddie Fisher akijichukulia mazima Sue Kennedy.

Chanzo: michelemalkin.com

Kifo Cha Bakari Abeid Na Urithi Wa Mswahili

Utunzi wa Marehemu Bakari Abeid


Gwiji La Kughani Marehemu Seif Salum

Bakari Abeid Gwiji La Sanaa Z'bar Afariki Dunia

Marehemu Bakari Abeid
  Marehemu Bakari Abeid(1933-2010)

Na Salum Vuai
KAMBI ya wasanii wa fani za taarab na maigizo nchini, imegubikwa na msiba kwa kuondokewa na msanii gwiji na mkongwe Bakari Abeid Ali aliyefariki jana alfajiri nyumbani kwake Mombasa mbuyu mnene.

Marehemu huyo (77) amekutwa na mauti baada ya kukumbwa na maradhi ya kiharusi yaliyomsumbua kwa muda mrefu.

Msanii huyo aliyezaliwa Agosti 25, 1933 katika kijiji cha Ole kisiwani Pemba, atakumbukwa kwa umahiri wake katika sanaa za utunzi, uimbaji taarab na maigizo, ambapo aliweza kuwavutia mashabiki wengi katika ukanda huu wa Afrika Mashariki.

Wakati wa uhai wake katika enzi alizojikita kikamilifu katika usanii, Abeid alikuwa hodari wa kuwatuliza watazamaji alipokuwa jukwaani kwa namna alivyomudu kuiteka hadhira kwa umahiri wake wa kuigiza na kuimba.

Baada ya kudhihirisha kipaji chake, marehemu aliwahi kuwa mwanachama wa vyama tafauti vya taarab ikiwemo Michenzani alichoshiriki kukiasisi mwaka 1952, Nadi Ikhwan Safaa (1956) na Culture (1964).

Akiwa msanii mashuhuri, marehemu alishiriki kutunga na kuimba au kutia muziki nyimbo mbalimbali katika vikundi hivyo na miongoni mwa hizo ni ‘Mazowea yana tabu’, ‘Njiwa peleka salamu’, ‘Tini tunda la tamasha’, ‘Pendo halijui siri’, ‘Bahati’, ‘Kisebusebu’, ‘Wagombanao hupatana’, ‘Nnapenda kwa ishara’ na nyengine nyingi.

Mbali na shughuli za kisanii, marehemu Bakari Abeid alifanya kazi serikalini na kushika nyadhifa kadhaa kwa vipindi tafauti kama vile Afisa wa Sanaa katika Wizara ya Habari, Utamaduni na Utalii (1985), Mjumbe wa Baraza la Sanaa Tanzania (1986), Mjumbe Baraza la Sanaa Zanzibar (BASAZA) mwaka 1989.

Aidha aliwahi kuwa Mkuu wa Habari, na baadae wa utangazaji katika Idara ya Habari na Utangazaji Zanzibar, Mkuu wa Vipindi Televisheni Zanzibar na Mshauri wa Rais mambo ya utamaduni na pia mshereheshaji mkuu katika sherehe mbalimbali za kitaifa.

Wananchi wengi watamkumbuka kwa kipindi kilichompatia umaarufu mkubwa katikaSauti ya Tanzania Zanzibar cha ‘Ndivyo tulivyo, akishirikiana na Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharibi Abdallah Mwinyi Khamis ambacho baadae kilihamia Televisheni Zanzibar.

Marehemu aliyezikwa jana katika makaburi ya Mwanakwerekwe ambapo mazishi yake yalihudhuriwa na mamia ya wananchi wakiwemo wasanii wa fani mbalimbali, ameacha mtoto mmoja wa kiume.

Gazeti la SMZ.na Mzalendo

Obama Na Odinga Mpira Kati

Odinga: Hii  Imekaaje



Obama:Dini Au Dunia

WikiLeaks:Kenya Yaifokea Marekani

Wakuu wa Serikali Ya Umoja wa Kitaifa wa Kenya wapuuzia taarifa ya WIILEAKS
 
 Waziri Mkuu wa Kenya Raila Odinga Akizungumza jambo,huku pembeni yake
 Rais Mwai Kibaki akimsikiza.

Serikali ya Kenya imepuuzilia mbali taarifa zilizofichuliwa na tovuti ya Wikileaks ambazo zinamnukuu balozi wa Marekani nchini humo, Micheal Rannenberger, akisema kwamba Rais Mwai Kibaki na waziri mkuu Raila Odinga ndio kikwazo kikuu katika kuleta mageuzi nchini Kenya.


Balozi huyo pia alinukuliwa akisema serikali ya Marekani haitasita kuendesha kampeni kupitia makundi ya kiraia ili kuhakikisha mabadiliko yanafanyika.

Akizungumza na BBC akiwa jijini London, Waziri Mkuu wa Kenya Raila Odinga amemshutumu bwana Rannenberger kwa kuwa mnafiki. ''Taarifa zinazotolewa na WikiLeaks ni uvumi mtupu. Yale yote yaliyomo ni masengenyo. Ni watu wanaokusengenya, wanayozungumza kukuhusu hadharani ni tofauti na yale wanayozungumza kisiri,'' akasema bwana Raila.

Kuhusu madai kuwa yeye na rais Kibaki hawakuchukuwa hatua zozote kwa kutekeleza mageuzi yanayohitajika, ili kuhakikisha kuwa machafuko ya baada ya uchaguzi kama yale yaliyoshuhudiwa baada ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2007 yatokee tena bw Raila amesema, '' Bwana Ranneberger anaishi nchini Kenya kama mgeni. Iwapo anataka kutushauri ana haki ya kufanya hivyo. Lakini vile vile wageni ni sharti watuheshimu''.

Nayo taarifa kutoka ikulu ya rais ya Nairobi imepuuzilia mbali madai hayo ya balozi wa Marekani kwa kusisitiza kuwa rais Mwai Kibaki ana historia nzuri ya kutekeleza mageuzi kwa kufanikisha kuidhinisha kwa katiba mpya ya taifa hilo.

Taarifa hizo za kisiri, ni miongoni mwa stakabadhi ambazo zimefichuliwa na tovuti ya Wikileaks , kuhusiana na nchi ya Kenya na viongozi wake.
Chanzo: BBC

Vibaka Watishia Raia Ubalozi Wa China Dar

BAADHI ya wafanyakazi wa ubalozi wa China , jijini Dar es Salaam, wanadaiwa kushirikiana na wezi wa kuvunja magari ya watu wanaofika ubalozini hapo.

Kumekuwa na matukio ya uhalifu katika ubalozi huo na Tanzania Daima ilifika katika eneo na kukuta vijana wakizagaa hovyo nje ya jengo la ubalozi hasa katika eneo la maegesho ya magari ambako uhalifu huo unafanyika.

Kadhalika ulinzi katika ubalozi huo uko ndani tu hali ambayo husababisha usumbufu na hasara kwa watu ambao wanakwenda katika ubalozi huo kwa shughuli za kikazi na kuegesha magari yao nje.

Wakizungumza na gazeti hili, baadhi ya watu ambao wamekumbwa na mkasa wa kuibiwa katika eneo hilo la maegesho ya magari ubalozini hapo walisema watu wanaofanya uhalifu huo ni wa rika tofauti tofauti na wamekuwa wakivinjari katika ubalozi huo bila shughuli yoyote muhimu.

Katika tukio la hivi karibuni, gari la Mkurugenzi Mtendaji na mmiliki wa maduka ya vipodozi ya Shear Illusions Shekha Nasser, lilivunjwa na kuibiwa Laptop moja, fedha taslimu kiasi cha sh 250,000, tiketi ya ndege moja na vitabu vya hundi viwili vya benki ya CRDB na NMB, funguo za maduka na vitu vingine mbalimbali.

Shekha alisema tayari amefungua jalada lenye RB OB/RB/21477/2010 katika kituo cha Polisi Oysterbay, Dar es Salaam.

Kwa mujibu wa Shekha, mara baada ya kuibiwa alimueleza mlinzi aliyekuwepo katika ubalozi huo, lakini jambo la kushangaza alimjibu kuwa hashangazwi na tukio hilo kwani vitendo hivyo vimeota mizizi na kukiri kwamba kwa siku huwa watu watano hadi sita huibiwa na kazi ya kulinda magari siyo ya kwao bali ni ya Jeshi la Polisi.

Tanzania Daima ilifanikiwa kufika eneo la ubalozi huo uliopo katika maeneo ya Oysterbay na kushuhudia hali ya hatari nje ya ubalozi kutokana na kukosekana ulinzi kama zilivyo balozi nyingine.

Kadhalika watu wanaoranda randa katika ubalozi huo wanadai kuwa wao ni mawakala wa kusaidia watu kupata pasi za kusafiria.

Chanzo: Tanzania Daima

Friday, December 10, 2010

Maadhimisho Ya Miaka 49 Ya Uhuru Wa Tanzania

Halaiki Ya Ngoma


Uhuru Parade

Obama Kupigania Haki Za Mashoga

Rais Barack Obama amesema atahakikisha baraza la seneta la Marekani linafuta sheria inayowabana mashoga kujiunga na jeshi.Obama alitetea kwa kusema"sheria hii inadhoofisha usalama wa taifa,kuondoa utayari jeshini,na ni kinyume cha mfumo wa Marekani  kuhusu usawa ,uadilifu na haki".Amesema "haitakuwa ndiyo mwisho wa juhudi zao, kwani niliahidi kuiondoa sheria hii ya unyanyasaji".

Siku ya Jumatano ,Maseneta wa Republicans walizuia jitihada za kufuta sheria hii ya "usiulize,usiseme" inayowabana mashoga kujiunga katika huduma za wazi za kijeshi.Obama ,siku ya Alhamisi amewataka wajumbe wa seneta kufikiria tena uamuzi huo kabla  ya mwisho wa mwaka .

Matokeo ya kura yalikuwa 57-40,ni uchache wa kura 60 zinazohitajika ambazo chama cha Democratic kingeweza kushinda juhudi za chama cha Republican kuzuia sheria hiyo iliyodumu kwa miaka 17.

Robert Gates,Waziri wa Ulinzi wa Marekani kwenye utawala wa George Bush na Barack Obama aliwataka wajumbe kwa kuwauliza kama "sio sasa hivi? ,ni lini?" na Mike Mullen mwenyekiti wa maafisa jeshini ameunga mkono kufutwa sheria hiyo.

Takribani wanajeshi 13000 wanaume na wanawake walijitoa jeshini kutokana na sheria hii inayowabana mashoga kuto dhihirisha uhalisia wao pindi wakilitumikia jeshi.Tawimu zinaonesha kuna uungwaji mzuri toka jeshini kwa ufutwaji wa sheria hii.

Sheria hii ya "usiulize,usiseme" ilipitishwa rasmi mwaka 1993 na chama cha Democratic wakati wa utawala wa Bill Cliton.

Habari zaidi zinapasha kuwa Rais Obama amefanya makubaliano na chama cha Republican na kukubali kufuata sheria ya kodi ya utawala wa Rais George Bush.Katika makubaliano hayo utawapendelea zaidi watu wenye kipato cha juu kupata punguzo la kodi.

Obama ameonesha kutokubaliana na uendeleaji wa punguzo la kodi kwa watu matajiri,na kusema ni muhimu kutafuta suluhisho litakalo saidia walipa kodi wakipato cha kati wasilipe kodi zaidi ifikapo januari mwakani.

Kwa kufanya  hivyo,Obama anajaribu kuweka hali sawa kwenye ubaya.Maafisa wa serikali wanasema obama anaweka picha ya kuwa kiongozi mwenye kukubaliana na umoja wa vyama kwani ni muhimu katika kipindi hiki cha miaka miwili ijayo ya utawala wake kwani ni juhudi ya kutaka kuchaguliwa kwa mara nyengine.

Maseneta wa Republican wameahidi kutopitisha muswada wowote isipokuwa ule wa kuruhusu fedha serikalini ili kuweza kusaidia mamilioni ya wa amerika  hadi pale sheria ya punguzo la kodi kwa wenye kipato cha juu itakapo maliza muda wake.

Chanzo: aljazeera

AU Yaisimamisha Ivory Coast Uanachama

Shinikizo la kumtaka Rais Laurent Gbagbo wa Cote d'Ivoire kujiuzulu kufuatia mabishano yaliyozuka katika uchaguzi wa rais nchini humo limepamba moto hii leo, baada ya viongozi duniani kumzuia na wapinzani wake wa ndani kutaka jeshi liwatii.


Baada ya Umoja wa Afrika kuisimamisha Cote d'Ivoire uwanachama na Marekani kuonya kuiwekea vikwazo, utawala ulioanzishwa na mpinzani wake, Alassane Ouattara, umelitaka jeshi kumtambua yeye kama mkuu wa nchi hiyo. Taarifa iliyotolewa na serikali ya Ouattara imevitaka vikosi vya usalama na jeshi kuendesha shughuli zake kwa kufuata maagizo ya Ouattara, ambaye ni amiri jeshi mkuu.

Wito huo unazidi katika jitihada za kumbana Gbagbo ambaye anakabiliwa na hatua ya kutengwa huku kukiwa na shinikizo la kumtaka aachie madaraka kutoka kwa nchi zenye nguvu duniani, likiwemo Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, Umoja wa Afrika na wadau wengine muhimu wa kikanda. Mapema serikali ya Ouattara ilisema kutakuwa na utawala wenye ufanisi nchini Cote d'Ivoire, lakini Gbagbo bado hajalizungumzia suala hilo na wananchi wa Cote d'Ivoire wanasubiri kwa hamu hatua yake itakayofuata.
Chanzo: Dw

Thursday, December 9, 2010

Sherehe Za Miaka 49 Ya Tanzania

                          Rais Dr.Jakaya Mrisho Kikwete,akipunga mkono kuwasalimia
                          wananchi wakati alipokuwa akiingia Uwanja wa Uhuru Dar

                                        Rais Dkt.Jakaya Kikwete,akikagua gwaride

     Rais Dk Jakaya Kikwete, akisalimiana na Makamu wake,
                     Dk Mohamed Gharib Bilal. wakati alipokuwa akiingia uwanjani hapoRais Dk Jakaya Kikwete, akisalimiana na Makamu wa kwanza wa Rais wa Zanzibar,Maalim Seif na baadhi ya viongozi wa Serikali, alipoingia uwanjani hapoPicha Zote na Fersddy Maro
                                          

Dkt Robert Ouko 'Aliuwawa Ikulu'


Dkt.Robert Ouko,waziri wa zamani wa mashauri
ya nchi za kigeni Kenya,ripoti ya mauaji yake
imechukua miaka mitano kutayarishwa hadi jana
ilipokabidhiwa..

Ripoti iliyotarishwa na kamati ya bunge la Kenya miaka mitano iliyopita imedai kuwa aliyekuwa waziri wa mashauri ya nchi za kigeni aliyekuwa na ushawishi mkubwa Robert Ouko, aliuwawa katika ikulu ya rais mjini Nakuru.


Ripoti hiyo iliyotayarishwa na kundi la wabunge wa Kenya inadai kuwa Bwana Ouko aliuwawa baada ya kutofautiana na waziri mwenzake katika serikali ya rais mustaafu Daniel Arap Moi wakiwa ziarani nchini Marekani.

Ripoti hiyo iliwasilishwa katika bunge la Kenya siku ya Jumatano. Ripoti hiyo inapendekeza kuchunguzwa kwa watu mashuhuri waliohudumu katika serikali ya rais mustaafu Daniel Arap Moi, wanaodaiwa kuhusika katika mauaji ya bwana Ouko.

Rais Mustaafu wa Kenya Daniel Arap Moi. Dkt. Robert Ouko aliuwawa wakati wa utawala wake.

Kadhalika ripoti hiyo inadai kuwa Bwana Ouko aliyeuwawa mwaka 1990, alikuwa tayari amefutwa kazi na walinzi wake kuondolewa juma moja kabla ya kutoweka kwake.

Ripoti hiyo inadai kuwa ubishi uliibuka kati ya Bwana. Ouko na waziri mwenzake baada ya waziri huyo kumkejeli kwa kumwita Ouko ''Bwana Rais''.

Mauaji ya Bwana Ouko yalizua tetesi kali nchini Kenya na ni mojawepo tu ya mauaji mengi ya kisiasa yanayodaiwa kutekelezwa na serikali ya Kenya tangu taifa hilo lijinyakulie uhuru mwaka 1963.

Uchunguzi wa kina wa mauaji hayo bado haujakamilika huku mfumo wa sheria nchini humo ukilaumiwa kwa kuwa kizingiti cha kupatikana .
Chanzo: BBC Swahili

Miaka 49 Ya Uhuru wa Tanganyika



Wosia wa Mwalimu Nyerere


Nyerere Muungano


Kwa video zaidi za harakati wa Uhuru wa Tanganyika
tizama: http://www.britishpathe.com/record.php?id=81710

Wednesday, December 8, 2010

Does Nigeria Have a Case Against Dick Cheney?

Nigerian officials have indicted former Vice President Dick Cheney for bribing the Nigerian government in the '90s. The accusation stems from Cheney's reign as CEO of Halliburton from 1995 to 2000, and the investigation has been going on for a while. In 2009, KBR, a subsidiary of Halliburton, plead guilty in U.S. courts to paying bribes from 1995 to 2004 in order to build a liquefied natural gas plant in Niger Delta. While a number of liberals are salivating at the notion of Cheney locked up in a Nigerian prison, few predict that the U.S. will ever agree to extradite him. Additionally, it doesn't help that Nigeria happens to be one of the most corrupt governments in the world.

Uhuru Wa Vyombo Vya Habari Wakabiliwa na Mtihani

Kesi ya Asange ni kitisho kwa uhuru wa vyombo vya habari

Baada ya wiki kadhaa za vuta nikuvute, muanzilishi wa Wikileaks Julian Assange amejisalimisha kwa polisi ya Uingereza. Bwana Assange anakabiliwa hasa na tuhuma za ubakaji nchini Sweden. Inasemekana pia kua Marekani ingependa kukapidhiwa Bwana Assange ili afikishwe mbele ya mahakama ya nchi hio, kwa mashtaka ya ujasusi.

Habari muhimu na za siri zinazotangazwa na mtandao wa Wikileaks zinavyoenea haraka, ndivyo shida za kibinafsi za muanzilishi wa Wikileaks, Bwana Julian Assange, raia wa Australia zinavyoelekea kua mzozo wa kisiasa wa kimataifa.

Hakuna anaejua kikamilifu, nini kilichotokea usiku wa siku hizi mbili za mwezi ogosti nchini Seeden; zinazohusishwa na tuhuma dhidi ya Bwana Assange.

Lakini inaelekea ofisi ya mwendesha mashtaka wa nchi hio haikuweza kuelewa kivingine mazingira ya shida zinazomkabili Bwana Assange, kama si mkono wa serikali ya Marekani dhidi ya Wikileaks.

Kwa taifa kubwa kama Marekani, taarifa za Wikileaks zimekua tukio lililoikera sana na haijafurahia kushuhudia, vipi kundi dogo tu lilivyozifichua siri zake muhimu kwa dunia nzima, bila kujua ifanye nini.

Ilianzia shida za Marekani katika vita vyake vya Afganistan, ikaja mikasa ya vita vya Irak, na hatimae ujumbe mbali mbali wa kidiplomasia baina ya maafisa wa wizara ya mambo ya kigeni wa Marekani.

Taarifa za wikileaks zimeathiri sura ya Marekani katika nchi za nje. Lakini, ni kipya ambacho mtu alikisoma katika habari hizo za Wikileaks kuhusu Afganistan ambacho kilikua hakijulikani tangu zamani? Nini ambacho wataalamu wa Afganistan walikua hawajasema. Kuna chochote kipya ambacho kinatupatia nafasi ya kukosoa mtazamo wetu kuhusu vita vya Irak?

Bila shaka ni jambo la kuchukiza, kwamba maafisa wa kidiplomasia wa Marekani wamejikuta katika hali ambayo wanabidi kuomba msamaha kwa kuhusika na ujumbe uliosababisha madhara. Lakini je, madhara gani.

Madhara yanaweza kuzungumzwa kwa mfano, wakati ambapo Waziri wa mambo ya kigeni wa Marekani Hillary Clinton, katika ujumbe uliopewa jina la "Cablegate" anapodai kuwepo "hujuma dhidi ya jumuia ya kimataifa". Au wakati ambapo Bwana Assange anapotuhumiwa kua msaliti, gaidi na muhalifu mkubwa.

Madhara yanakuwepo wakati mtandao wa kulipia wa Paypal Wikileaks unapokuwea huwezi kutumiwa, Kadi za benki za kulipia zinakuwa haziwezi kutumiwa, au wakati mfumo mzima wa malipo kwa kutumia Amazon Wikileaks unapofutwa.

Kwa vyovyote vile, uhuru wa maoni unalindwa na mahakama kuu ya Marekani, na umefafanuliwa zaidi hata kuliko ilivyo hapa Ujerumani. Lakini sasa swali hili kuhusu uhuru wa maoni nchini Marekani, linaulizwa pia katika mitandao ya Internet nchini China, kwamba kwa umbali gani kuna uhuru wa maoni nchini Marekani?
Chanzo:Dw

Jumuiya Ya ECOWAS Yamtambua Ouattara Kama Rais Wa Cote d´Ivoire

Jumuiya ya Kiuchumi ya nchi za Afrika magharibi ECOWAS wamemtambua Alassane Ouattara kama Rais aliyechaguliwa nchini Cote d'Ivoire na kumtaka rais Laurent Gbagbo kukubali kushindwa .

Baada ya mkutano wa dharura uliohudhuriwa na viongozi wa mataifa ya kanda hiyo, uliofanyika Abuja Nigeria, Jumuiya hiyo ya ECOWAS imemuongezea mbinyo zaidi Bwana Gbagbo kwa kuisimamisha nchi hiyo kujihusisha na kundi hilo.

Aidha, Rais wa muda wa ECOWAS, Rais wa Nigeria Goodluck Jonathan ameonya dhidi ya juhudi za kuzuia makubaliano hayo, kama ilivyotokea nchini Kenya na Zimbabwe.

Awali Bwana Gbagbo alikataa kutekeleza matakwa ya kimataifa, ya kumtaka kukubali kushindwa na badala yake kutangaza baraza lake la mawaziri, ikiwa ni siku mbili tu baada ya mpinzani wake Alassane Ouattara kutangaza pia serikali yake, chini ya ulinzi wa kikosi cha kulinda amani cha Umoja wa Mataifa. Jana Gbagbo alifanya kikao cha kwanza cha baraza lake la mawaziri.

Mabishano yaliyozuka kufuatia matokeo ya uchaguzi wa rais nchini humo mwezi uliopita katika nchi hiyo iliyo maarufu kwa zao la kakao, yamezidisha hatari ya kutokea tena ghasia katika taifa hilo ambalo bado limegawanyika baada ya vita vya wenyewe kwa wenyewe vya mwaka 2002 na 2003, hali iliyosababisha pia Umoja wa Mataifa kuondoa baadhi ya wafanyakazi wake.

Kwa mujibu wa shirika la Kimataifa la Msalaba mwekundu, mapigano kati ya majeshi ya ulinzi na kati ya wafuasi wanaopingana wa viongozi hao yamesababisha vifo vya watu 28 na wengine 280 kujeruhiwa tangu Novemba 26.

Wakati huo huo, Katika Umoja wa mataifa wanadiplomasia wanasema kuwa Urusi imeipinga taarifa iliyotolewa ya kumtambua Alassane Ouattara kama Rais wa Cote d'Ivoire.Wanadiplomasia wamearifu kuwa baada ya mazungumzo ya faragha yaliyodumu kwa takriban saa tano na nusu, mazungumzo hayo yaliahirishwa kwa siku kwa wajumbe wa Urusi kusema kwamba wanahitaji maelekezo zaidi kutoka Moscow.

Nafasi ya Urusi ni nguzo kubwa kwa sababu taarifa za Baraza la Usalama la Umoja wa mataifa lazima ipitishwe na wote bila ya kupingwa, ikiwa na maana kuwa mwanachama yeyote akipinga maamuzi yaliyofikiwa atazuia hatua hiyo.

Balozi wa Marekani katika Umoja wa Mataifa,Susan Rice, ambaye kwa sasa ndiye rais wa mwezi wa baraza hilo amesema ana matumaini kuwa mjadala huo utaendelea leo.

Kwa upande wake, mkuu wa Ujumbe wa Umoja wa Mataifa katika Afrika magharibi Y J Chio amethibitisha kuwa Ouattara ndiye mshindi, ambapo alilifahamisha baraza la usalama pia kwamba matokeo ya uchaguzi yalikuwa wazi na kwamba kulikuwa na mshindi mmoja tu.

Awali akithibitisha hilo alisema, '' Matokeo yamethibitisha tena Bwana Ouattara kuwa ni mshindi wa duru ya pili ya uchaguzi wa Rais wa Cote d'Ivoire.''
Kuidhinishwa huko kwa Bwana Ouattara na Umoja wa mataifa kumemfanya Bwana Gbagbo kuwa na wafuasi wachache kimataifa baada ya jumuia ya ECOWAS pia kumtambua Ouattara.
Chanzo:DW

Tuesday, December 7, 2010

Wahisani Bajeti Tuliyopewa Ni Tofauti Na Iliyosomwa Bungeni

KUNDI la wahisani wanaochangia bajeti kuu ya Tanzania (GBS) limeibua kashfa baada ya kueleza kuwa serikali iliwapelekea bajeti tofauti na ile iliyopitishwa na Bunge Julai mwaka huu.Taarifa za kashfa hiyo ziliwekwa hadharani jana asubuhi na mwenyekiti wa wahisani hao, Svein Baera wa Sweden katika mkutano wa kitaifa wa mwaka wa majadiliano ya kisera na bajeti uliofanyika jijini Dar es salaam.

Sweden ndiyo inayoshikilia uenyekiti wa kundi hilo linalojumuisha taasisi za kimataifa na nchi mbalimbali zilizoendelea.

Kuibuliwa kwa kashfa hiyo kunakuja wakati wahisani hao wakiwa wamezuia theluthi moja ya zaidi ya dola 800 milioni za Kimarekani ambazo zinatakiwa zichangie kwenye bajeti kuu ya 2010/11, wakiishinikiza serikali iharakishe utekelezaji wa programu ya mageuzi, yakiwemo ya mfumo wa usimamizi wa fedha za seikali.

Akitoa hotuba yake ya ufunguzi wa mkutano huo wa siku tatu, Baera aliainisha maeneo sita kuwa ndiyo mhimili wa mjadala wao na serikali.

"Napenda kuainisha maeneo sita ya ujumbe wetu ili kuweka sawa jukwaa la majadiliano yetu haya ya mwaka. Kuna tofauti kati ya bajeti iliyowasilishwa kwa bodi ya (Shirika la Kimataifa la Fedha) IMF na ile iliyopitishwa na Bunge Julai 2010," alisema Baera.

Alisema bajeti ambayo serikali iliwasilisha kwa wahisani hao ilibeba "matumaini makubwa ya kuzaa matokeo mazuri na kufanywa kama sababu ya kupitisha matumizi makubwa ya fedha zitokanazo na mapato ya ndani".

Baera alisema kuwa kukosekana kwa uwazi katika matumizi, vipaumbele, mapato na mfumo mzima wa fedha kunapunguza kuaminika kwa bajeti hiyo mbele ya wafadhili.

Kwa mujibu wa wahisani hao, kumekuwepo na mtiririko wa athari katika bajeti katika miaka ya karibuni huku ikionyesha ongezeko kubwa la matumizi ya kawaida kuliko yale ya maendeleo.

Kwa mujibu wa bajeti ya mwaka 2010/11 ambayo ni ya Sh11.1 trilioni, matumizi ya kawaida ya serikali ni Sh7.8 trilioni wakati fedha zilizotengwa kwa ajili ya shughuli za maendeleo ni Sh3.2 trilioni.

Bajeti hiyo inaonyesha kuwa kati ya Sh11.1 trilioni, serikali ilitarajia kupata Sh6 trilioni kutoka katika vyanzo vya ndani, wakati inatarajia Sh2.8 trilioni kutoka kwa wahisani na mikopo. Fedha nyingine zinatarajiwa kutoka mikopo ya ndani, masharti ya kibiashara na ubinafsishaji.

"Matumaini makubwa kupindukia katika bajeti hii na kutokuwepo kwa mikakati inayoeleweka ya kipaumbele katika matumizi katika hali inayoweza kutokea ya mapato madogo na ukosefu wa fedha, yanaweza kuondoa kuaminika kwa bajeti kama chombo cha ufanisi wa sera na mipango," alisema Baera.

Zaidi ya hapo, ukweli kwamba bajeti hii tofauti ilipitishwa bila ya kuwepo mawasiliano ya awali na wabia wa maendeleo inaweka maswali kwenye ubora wa mazungumzo yetu ya sera na ubia. Tunatarajia kujadili suala hili kwenye sehemu muhimu ya bajeti.

"Zaidi ya hapo, bajeti iliyotumiwa kuanzia mwaka jana iliendeleza mwenendo wa miaka ya karibuni ambako matumizi ya kawaida yanaendelea kupanda kwa kasi kuliko matumizi kwenye maendeleo."
Kutokana na hali hiyo GBS imeitaka serikali kujipanga upya na kuweka mkazo katika kupunguza misamaha ya kodi ili kuweka uwiano na ufanisi sawa na nchi za kundi lake katika uchumi, hatua ambayo Baera alisema itapunguza pengo la bajeti linaloikabili Tanzania kila mwaka.

Tayari GBS imebainisha kuwa bajeti ijayo inaweza kuwa na nakisi ya hadi Sh1 bilioni.

Hata hivyo, Waziri wa Fedha na Uchumi, Mustafa Mkulo ambaye alishiriki mkutano huo, alipatwa na kigugumizi kujibu madai hayo ya GBS, akimkaribisha mwenyekiti huyo wa kundi la nchi wahisani aende ofisini kwake ili wazungumzie masuala hayo.

"Kuna mengine yanazungumzika; Baera ninakukaribisha ofisini kwangu; mengine yanazungumzika ofisini," alisema Mkulo.

Naibu kiongozi wa kambi ya upinzani bungeni, Zitto Kabwe alizungumzia kasoro hiyo jana akieleza kuwa imemshtua na kwamba ataifuatilia.

Zitto, ambaye pia ni mbunge wa Kigoma Kaskazini na ambaye alihudhuria mkutano huo jana, alisema kambi ya upinzani itaunda kamati kulifuatilia suala hilo.

Alisema pia watahoji suala hilo bungeni na kuitaka serikali iweke wazi kwa Watanzania ni bajeti ipi inayotumika kati ya iliyopitishwa na Bunge na ile iliyopelekwa IMF.

"Huu ni mshtuko kwangu; hili limenishtua. Tutaunda timu ya kulifuatilia; tutalifikisha bungeni na kuihoji serikali ieleze ni bajeti ipi inayotumika. Ni ile iliyopitishwa na Bunge au iliyopelekwa IMF," alisema Zitto.

Kundi hilo la nchi wahisni limesema kuwa linaunga mkono mkakati wa serikali wa Kilimo Kwanza na wa Jumuia ya Afrika Mashariki (EAC) kuhusu maendeleo ya kilimo, hifadhi ya chakula na kupunguza umasikini.

Chanzo:Mwananchi

Dk. Shein Asita Kuwaapisha Majaji

RAIS wa Zanzibar Dk. Ali Mohammed Shein amekuwa akisitasita kuwaapisha majaji wanne aliowateua Novemba 29 mwaka huu kufuatia barua aliyoandikiwa na Chama Cha Mawakili Zanzibar (ZLS) juu ya uteuzi huo kutozingatia taratibu. Kusita huko kwa Dk. Shein kuwaapisha tangu awateue, kunaelezwa kuwa kunatokana na utata wa kisheria uliopo kutokana na majaji hao kutoiva vya kutosha katika taaluma ya sheria na kwa mujibu wa sheria tume ya utumishi ilipaswa kukaa kuidhinisha majina hayo jambo ambalo halikufanywa kwa baadhi ya majaji walioteuliwa.


Baadhi ya mawakili wakiongozwa na rais wa chama cha mawakili Zanzibar, Yahya Khamis Hamad waliosaini barua ya kumpinga Dk Shein juu ya uteuzi wa majaji hao ambao kwa mujibu wa maelezo yao hawana sifa zinazowafanya wawe majaji wa mahakama kuu.

Rais wa Zanzibar kwa mamlaka aliyopewa alifanya uteuzi wa majaji wanne wa Mahakama Kuu pamoja na Mwenyekiti wa Mahkama ya Ardhi ambaye ni Haroub Sheikh Pandu, na majaji wanne wa mahakama kuu akiwemo Abdul-hakim Ameir Issa, Fatma Hamid Mahmoud, Mkusa Isaac Sepetu, na Rabia Hussein Mohammed.

Chama hicho kilisema uteuzi huo, ulikuwa unatumia mamlaka aliyopewa rais na Katiba ya Zanzibar, 1984 kifungu cha 94(2) na (3) ambapo Chama cha Mawakili hakina mashaka na uteuzi wa Abdul-hakim Ameir Issa, wala uteuzi wa Mwenyekiti wa Mahakama ya Ardhi, Haroub Shehe Pandu.

Chama hicho kilisema kuwa mashaka yapo kwa Fatma ambaye ni mtoto wake Jaji Mkuu wa Zanzibar, Mkusa Isaac Sepetu na Rabia Hussein Mohammed ambao wote watatu wanadaiwa kutokuwa na sifa zinazostahiki kuteuliwa nafasi hiyo.

Juzi Disemba tatu usiku Jaji Mkuu wa Zanzibar, Hamid Mahmoud aliitisha kikao cha tume ya utumishi ambacho anadaiwa kuwa hakikupitisha jina moja la jaji aliyeteuliwa na mawakili hao ili wajadiliane, lakini kikao hicho kilishindwa kufanyika baada ya kupokea barua nyengine kutoka chama cha mawakilishi kusema kwamba kikao kitakachofanyika hakitokuwa halali kwa mujibu wa sheria kwa kuwa wajumbe wa kikao hicho hawakutimia.

Kwa mujibu wa barua iliyosainiwa na katibu wa chama cha mawakili, Salim Mkonje iliyotumwa kwa rais wa Zanzibar ya Desemba tatu mwaka huu, ambayo tayari saini ya rais inaonesha ameshaipokea ilisema kwamba wakili Awadh Ali Said ambaye alikuwa mjumbe wa tume ya uajiri anayetokana na chama hicho katika vipindi viwili vimekwisha tokea septemba 17 mwaka huu hivyo hawezi kuwa mjumbe tena hadi hapo atakapoteuliwa tena.

Mbali na mjumbe huyo, lakini pia Jaji Mshibe Ali Bakari naye muda wake umekwisha kwa mujibu wa sheria ya tume hiyo No 13 ya mwaka 2003 koramu ni wajumbe watano kifungu cha 9(2).
“Kufutia kikwazo hiki wakili Awadh alifahamishwa na katibu wa tume ya uajiri ya mahakama asihudhurie kikao cha leo 3 Desemba jana usiku” ilisema barua hiyo kutoka kwa mawakili. Na kuongeza kwamba.
“Kwa sababu wajumbe waliokuwepo walikuwa sita hivyo kupungua kwa wajumbe wawili kunapelekea tume isiweze kufanya maamuzi kama sheria inavyotaka kwani yatakuwa batili kwa kukosekana koram,” alisema barua hiyo.

Aidha chama hicho kimeitisha kikao chake jana kuteuwa jina la wakili ambaye atakiwakilisha chama hicho na kulipeleka kwa rais ili ateuliwe kuingia katika kikao hicho ikiwa pamoja na wajumbe wengine ambao sheria inasema tume hiyo iwe na wajumbe wanane akiwemo jaji mkuu, mwanasheria mkuu na mwenyekiti wa tume ya utumishi, na kadhi mkuu.

Na Salma Said, Zanzibar, Mwananchi 6 Disemba 2010

Julian Asange Muasisi Wa Mtandao Wa Wikileaks Ajisalimisha

Katika kile kinachoonekana kuwa tayari kujibu tuhuma zinazomkabili ,Julian Asange ambaye anakabiliwa na kesi ya ubakaji nchini Sweden amejisalimisha katika mikono ya polisi wa uingereza.

Julian Asange ambaye mtandao wake wa Wikileaks umekuwa ni mwiba mchungu kwa Marekani na mataifa makubwa kwa kutoa kashfa za kijasusi, ameita kesi inayomkabili kuwa ni njama za Marekani.Mmoja wa mawakili wa bwana Asange, Mark Stephen amesema Sweden imepikwa na Marekani, ambayo imekuwa ikichukia kwa Wikileaks kutoa nyaraka za kiujasusi.
"Amesema swali ni kuwa Sweden inatumika na upande wa tatu au ni suala la uvunjaji wa taratibu za kimaingiliano."

Julian Asange anatarajiwa kufikishwa mahakama kuu ya Westminister jijini London siku ya jumanne , ambapo tarehe ya kusafirishwa  nchini Sweden itapangwa.
Chanzo:  http://english.aljazeera.net/news/europe/2010/12/2010127103159940201.html

Fungate Afrika Kusini Lageuka Mauaji

Katika hali isiyo kawaida bwana harusi amelipia mauaji ya mke wake, hayo yamejitokeza leo katika mahakama moja mjini capetown,Afrika kusini mara baada ya mtuhumiwa  wa mauaji  kukiri kulipwa sehemu ya makubaliano ili kutekeleza zoezi hilo la mauaji.

Zola Tongo ambaye ni dereva teksi amejitetea kwa kudai kuwa Shrein Dewan raia wa Uingereza alimuhadaa  ili amuue mke wake mpya Ani Dewan raia wa sweden siku baada ya kuwasili Afrika kusini.Mwili wa Ani Dewan ulipatikana siku ya pili katika kitongoji cha Gugulethu ambacho ni maarufu kwa uhalifu katika jiji la Capetown,Afrika kusini.Marehemu alikutwa ameuawa kwa risasi iliyopigwa toka nyuma ya shingo.

Tongo alidai kuwa Shrein Dewan alimtaka amtafutie mtu ambaye ataweza ufanikisha mauaji ya mke wake na kwamba atawalipa kila mmoja randi 50000(US$ 7000) lakini wamejikuta wakiambulia randi 1000(US$ 145).

Akiongea katika mahojiano na jarida moja nchini Uingereza ambalo kwa muda wa majuma kadhaa lilikuwa likimshutumu Shrein Dewan kwa mauaji hayo,msemaji wake alikana shutuma hizo.Na kwamba Shutuma zilizotolewa na dereva teksi kuwa Shrein alihusika katika mauaji ya mkewe  si kweli, kwani vithibitisho vya mwili wa marehemu vilivyotolewa  na polisi havikumuhusisha Shrein na mauaji hayo.Na kwamba mamlaka husika haikuwahi kuwasiliana na Shrein ambaye alirudi Uingereza mara baada ya mwili wa mkewe kupatikana.

Mthunzi Muhanga ,msemaji wa ofisi ya mshtaki mkuu wa Afrika kusini  amesema kutokana na ushahidi uliyojitokeza siku  ya jumanne suala la ombi  la kupelekwa Afrika kusini bwana Shrein linawezekana" jambo ambalo tunalifikiri kama sehemu ya uchunguzi unaoendelea.

Mtuhumiwa wa mauaji Zola Tongo amehukumiwa miaka 18,na anatarajiwa kutoa uthibitisho wa watuhumiwa wengine wawili ambao waliwekwa kizuizini mara baada ya mauaji ya Ani Dewan.

Akitoka nje ya mahakama huku akibubujikwa na machozi Mzazi wa Marehemu Ani Dewan,Bwana Vinod Hindocha ambaye alikuwepo wakati wa hukumu hiyo aliishukuru mamlaka ya Afria kusini iliyofanya uchunguzi wa kesi hii ,wananchi wa Afrika kusini na watu wote duniani walioiunga mkono familia yake.

Monday, December 6, 2010

Ouattara amtaka rais wa Côte d'Ivoire Laurent Gbagbo ajiuzulu

Rais wa zamani wa Afrika Kusini Thabo Mbeki yumo mjini Abidjan kuongoza juhudi za upatanishi, huku jeshi la Côte d'Ivoire, likiifungua mipaka ya anga, majini na ardhini ya taifa hilo

Kiongozi wa upinzani nchini Côte d'Ivoire, Alassane Ouattara, ambaye anadai ndiye rais mpya wa nchi hiyo, amesema rais wa sasa Laurent Gbagbo lazima ajiuzulu baada ya uchaguzi uliozusha mzozo nchini humo. Ouattara ameyasema hayo baada ya kukutana na rais wa zamani wa Afrika Kusini, Thabo Mbeki, anayeongoza juhudi za upatanishi nchini Côte d'Ivoire. Ouattara amemwambia Mbeki kwamba yeye ndiye rais halali wa Côte d'Ivoire na kumtaka amshawishi rais Gbagbo aondoke madarakani baada ya kushindwa katika uchaguzi. Bwana Mbeki aliyewasili jana mjini Abidjan amesema wanataka kusikiliza maoni yote kuhusu suala hilo kabla kutoa mapendekezo yoyote.


Ouattara ametangaza serikali yake na kumteua waziri mkuu wa zamani wa serikali ya Gbagbo, Guillaume Soro, kama waziri mkuu mpya atakayekuwa pia waziri wa ulinzi. Rais Gbagbo aliapishwa Jumamosi iliyopita ingawa tume ya uchaguzi ya Côte d'Ivoire ilimtangaza Ouattara kama mshindi wa uchaguzi wa Novemba 28 mwaka huu, matokeo ambayo yalithibitishwa na Umoja wa Mataifa. Wakati huo huo, jeshi la Côte d'Ivoire limetangaza kuwa mipaka yote ya nchi hiyo imefunguliwa kuanzia saa kumi na mbili asubuhi ya leo. Haikubainika wazi kwa nini jeshi hilo limeamua kuifungua mipaka wakati huu.
Chanzo:Dw Swahili

MAWAZIRI NI WA SMZ SIO WA CUF,CCM - BALOZI SEIF IDDI

• Ataka waache ushabiki, waweke mbele maslahi ya Nchi

Na Mwantanga Ame

MAKAMU wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali Iddi, amewatahadharisha Mawaziri walioteuliwa kuziongoza wizara za serikali kutekeleza wajibu wao wakizingatia kuwa ni mawaziri wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, na sio kufanya kazi kama Mawaziri wa vyama vya CCM na CUF.

Balozi Iddi, aliyasema hayo jana alipokuwa akifungua kongamano la kumbukumbu kumuenzi aliyekuwa Mkuu wa kituo cha huduma za Sheria Zanzibar marehemu Profesa Haroub Othman, iliyofanyika katika Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA) Mjini Zanzibar.

Alisema Zanzibar ina ushabiki mkubwa wa vyama, lakini haitakuwa busara kwa Mawaziri walioteuliwa wakaanza kufanya kazi zao kwa misimamo ya vyama vyao huku wakisahau kuwa wao ni viongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na sio CCM wala CUF.

Alisema Mawaziri hao wanatakiwa kuwajibika kwa maslahi ya nchi kwa vile wananchi wamejenga matumaini ya kuhudumiwa kwa kuzingatia kanuni za utawala bora zisizotoa nafasi kwa kiongozi kumuonea mtu kwa rangi yake, dini chama ama kijiji alichotoka.

Makamu huyo alisema mambo hayo ni ya msingi na yanahitaji kuzingatiwa na Mawaziri hao kwani ndio jambo pekee litaloiwezesha serikali ya Umoja wa kitaifa kufanya vizuri na dhana halisi ya kuwatumikia wananchi itaweza kufikiwa.
"Serikali ya Umoja wa kitaifa haishinikizwi na matokeo ya uchaguzi bali huundwa kwa nia njema kuaminiana na kwa ridhaa ya vyama husika kabla ya hata kuelekea kwenye zoezi la uchaguzi, msingi mkubwa ni kuweka mbele maslahi ya Zanzibar kuliko maslahi ya vyama vyetu, kijiji mtu anachotoka au maslahi binafsi”,alisema Makamu huyo.

Akiendelea alifahamisha kuwa mfumo wa serikali ya umoja wa kitaifa iliopo Zanzibar, inawataka Mawaziri waliotoka katika Chama cha CCM na CUF kujenga kuaminiana pamoja na kumuamini Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein kwa vile ndio mfumo waliouchagua kuutumia.

Alisema hivi sasa yapo baadhi ya maoni ya wasomi yanayodai kuwapo kwa muundo huo wa serikali kunaifanya serikali ilale usingizi kwa sababu hakuna upinzani wa kuikosoa serikali jambo ambalo halina ukweli kwani bado Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi wenye haki ya kuiohoji serikali.

Alisema lengo la serikali hiyo ni moja ya njia ya kuelekea katika demokrasia, ushirikiano katika kuendesha serikali, kupatikana utulivu wa kisiasa ili kuleta maendeleo ya nchi.

Akizungumzia dhana halisi ya kumbukumbu hiyo, alisema marehemu Profesa Haroub wakati wa uhai wake aliamini kwa dhati, amani, upendo na maendeleo yatakuja tu Zanzibar kama kutakuwa na utawala utaowajumuisha Wazanzibari wote.

Alisema dhana hiyo ya Profesa ilitokana na uzoefu alioupata wakati akisimamia uchaguzi wa kwanza katika mfumo wa vyama vingi alipokiongoza kikundi cha Zanzibar Election Monitoring and Observer Group' (ZEMOG) na ripoti yake kutoa mapendekezo kuwa serikali ya umoja ndio jawabu na kuondoa mivutano ya kisiasa.

"Jambo hili alilihubiri na kulieleza kwa nguvu zake zote kwa sababu aliamini, hivyo ni faraja kuona kwamba mwaka huu ndoto yake hiyo ya siku nyingi imetimia na kweli tayari tumeanza kuona matunda ya serikali ya Umoja wa Kitaifa katika nchi yetu" alisema Balozi Iddi.

Mapema Mwenyekiti wa Kituo cha Huduma za Sheria Zanzibar, Chris Peter Maina alisema mchango wa Profesa Haroub, wakati wa uhai wake tayari umeweza kuwanufaisha Wazanzibari kwa kupata huduma za sheria kupitia kituo hicho.

Nae mmoja wa Wawakilishi wa familia hiyo akitoa shukrani zao alisema wanaiunga mkono serikali iliopo madarakani kwani itaweza kuwatetea Wazanzibari katika maslahi ya Muungano na kinachohitajika ni kuweka kando ushabiki wa kisiasa.
Kongamano hilo liliwapa fursa washiriki mbali mbali kutoa michango yao juu ya mada ya Serikali ya umoja wa kitaifa iliyowasilishwa na Profesa Issa Shivji, akiwemo Waziri wa Nchi Afisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais Fatma Abdul-habib Ferej na Naibu Waziri wa Wizara ya Uhusiano wa Kimataifa Mahadhi Juma Maalim na wasomi, wanasheria viongozi wa vyama na wachambuzi wa mambo ya kisiasa

Sunday, December 5, 2010

Mzozo wa Ivory Coast

Nchi moja, Marais wawili ndivyo hali ilivyo nchini Ivory Coast
Wagombea wote wawili wa urais waapishwa,
huku hali ya wasiwasi ikongezeka

                                     
    Rais Laurent Bagbo,aliapishwa jana

Rais wa zamani wa Afrika Kusini Thabo Mbeki amewasili nchini Ivory Coast kujaribu kuleta upatanishi katika mzozo wa uchaguzi ambao ulitarajiwa kumaliza mzozo uliodumu nchini humo kwa muongo mmoja, lakini badala yake umeufanya mzozo huo kuwa mgumu zaidi. Hii ni baada ya wagombea urais wote kuapishwa. Rais wa sasa Laurent Gbagbo aliapishwa, licha ya tume ya uchaguzi kumtangaza Alassane Ouattara kama mshindi. Hata hivyo baada ya muda wa saa kadha, Ouattara ambaye ni mgombea wa
upinzani naye pia alidai kuwa rais. Marekani, Umoja wa Ulaya na Umoja wa Mataifa kwa pamoja zimesema kuwa mshindi wa uchaguzi wa Jumapili iliyopita ni Ouattara. Ouattara alitangazwa mshindi na tume ya uchaguzi lakini hatua hiyo ilibatilishwa na baraza la katiba la nchi hiyo, taasisi ambayo inaongozwa na mshirika wa rais Gbagbo. Uchaguzi huo ulikuwa na lengo la kupoza majeraha ya vita vya wenyewe kwa wenyewe vya mwaka 2002, lakini badala yake unatishia kuanzisha upya hali ya wasi wasi.
Chanzo: Dw swahili
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...