Mtazamohalisi

Tuesday, October 19, 2010

Kuondoka kwa Maghimbi hakujaiathiri CUF, asema Seif

Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi (CUF), Maalim Seif Sharif Hamad
Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi (CUF), Maalim Seif Sharif Hamad, amesema kitendo cha aliyekuwa Kiongozi wa Upinzani Bungeni kutoka chama hicho, Fatma Maghimbi, kuhamia CCM ni haki yake kidemokrasia, lakini hakina athari yoyote kwa chama hicho.
Akizungumza na wandishi wa habari mjini Zanzibar jana , alisema CUF hakijapata athari yoyote kisiasa kwa Maghimbi na aliyekuwa Mjumbe wa mkutano Mkuu wa chama hicho, Juma Othman Juma kuhamia CCM.

“Naweza kusema kwamba hatuoni kama tumepata pigo katika hilo, isipokuwa tunamtakia kila la heri katika maisha yake mapya ya kisiasa”, alisema Katibu Mkuu wa CUF.

Alisema kwamba CUF ipo imara na katika kudhihirisha hilo, majimbo yote 18 kisiwani Pemba yataendelea kushikiliwa na chama hicho cha upinzani.

Maghimbi na mwenzake wamekihama chama cha CUF na kuhamia CCM na walikabidhiwa kadi ya CCM na Mwenyekiti wa CCM, Rais Jakaya Kikwete katika mkutano wa hadhara uliofanyika Kawe jijini Dar es Salaam.

Maalim Seif alisema Maghimbi ambaye alikuwa Mbunge wa Chakechake amekihama CUF baada ya kukosa nafasi ya ubunge kufuatia wanachama kumkataa wakati wa kura ya maoni wakati wa mchakato wa kutafuta wagombea wa chama hicho kisiwani Pemba.

“Wapo watu chama kinakuwa kizuri pale wanapokuwa na madaraka wanapokosa chama kinakuwa kibaya, lakini kuondoka kwao hakutaacha pigo lolote kwa CUF, kwasababu hiki ni chama cha wananchi”, alisema Maalim Seif.

Alieleza kwamba tabia ya viongozi wanaokosa vyeo kuhama vyama sio ngeni, kwa vile wapo waliowahi kufanya vitendo kama vya Maghimbi na wamekiacha chama cha CUF kikizidi kuimarika.

Jijini Dar es Salaa, Naibu Mkurugenzi wa Uenezi na Mahusiano CUF, Ashura Mustapha, alisema Maghimbi hana tena mvuto wa kisiasa.

Alisema mwasisi huyo aliamua kukihama chama cha CUF baada ya kuona hana mvuto tena wa kisiasa.

“Ameamua kuhama kwa sababu anaona amepitwa na wakati na wananchi hawamtaki tena,” alisema.

“Maghimbi anadai eti ameamua kuhama CUF kutokana na Upemba kuzidi katika jimbo hilo, lakini tunaamini kuwa wananchi wenyewe ndio walioamua kufanya mabadiliko baada ya kuona hana mvuto tena wa kisiasa, na hata hivyo pia wanaangalia alama za nyakati upo muda wananchi pia wanahitaji mabadiliko,” alisema  Mustapha.

Alisema japokuwa Maghimbi ametumia Demokrasia kuhama chama, lakini pia ameonyesha ni jinsi gani uongozi wake haukua kwa manufaa kwa wananchi.

“Kama kweli Maghimbi hakuwa CUF kwa ajili ya kujinufaisha mwenyewe,asingeweza kuhama kwa kuanguka kipindi kimoja tu,wakati ameongoza kwa miaka kumi,” alisema.

Monday, October 18, 2010

Zijue sera za Chadema - Sehemu ya pili.

Zijue Sera za Chadema katika uchaguzi -October

Zijue sera za CCM Sehemu ya pili

Zijue Sera za CCM katika uchaguzi wa mwaka 2010

Zijue Sera za CUF katika uchaguzi 2010.

ITV na Habari za Tanzania

Mchakato wa wabunge Kigoma kusini.

Mchakato majimboni katika jimbo la Morogoro Mjini

Fatma Maghimbi Ajiunga Na CCM



- Kaongozana na Juma Othman Juma

- Waiaga CUF na kuchukua kadi za CCM

- Waahidi wengi zaidi wanakuja nyuma yao visiwani humo


Wakongwe wawili wa siasa za vyama vingi visiwani Zanzibar Mheshimiwa Fatma Maghimbi na Juma Othman Juma wamerudisha kadi zao za CUF na kuchukua za CCM jana jimboni Kawe jijini Dar es salaam na kuahidi wenzao wengi watafuata nyayo zao kutoka CUF.


Akielezea sababu zake za kurudi CCM, Juma Othman Juma amesema ameguswa kwa kazi kubwa aliyofanya Mheshimiwa Kikwete Tanzania Bara na Visiwani hususan aliporejesha amani na utulivu visiwani Unguja na Pemba kipindi cha uchaguzi mkuu wa mwaka huu.


Alisema tangu historia ya vyama vingi ianze Tanzania, kila wakati wa uchaguzi wananchi wengi wa visiwa vya Unguja na Pemba hulazimika kukimbia visiwani humo kwa kuhofia hali ya kutokuwa na usalama katika kipindi hicho.


"Lakini sasa napenda kumshukuru sana Mheshimiwa Kikwete kwa kurudisha heshima ya nchi yetu duniani kwani mwaka huu wa kampeni, hakuna hata mmoja aliyehama visiwani humo kukimbia uchaguzi" alimaliza Juma Othman akishangiliwa na umati mkubwa wa wana CCM waliojitokeza kwenye mkutano huo wa kampeni.


Mama Fatma Maghimbi amewahi kuwa waziri kivuli wa Katiba na Sheria ndani ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania akiwa kama mbunge wa Chama Cha Wananchi CUF. Naye Juma Othman Juma amewahi kuwa muanzilishi wa Chama Cha Siasa visiwani kabla ya kujiunga na Chama cha Wananchi CUF.

Pichani: Mgombea Urais wa Tanzania kupitia Chama Cha Mapinduzi Jakaya Mrisho Kikwete akimkaribisha Mama Fatma Magimbi CCM baada ya kurejesha kadi ya CUF kwenye mkutano wa kampeni jimboni Kawe Jijini Dar es salaam.
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...