Mtazamohalisi

Thursday, February 10, 2011

Wasanii na Upepo wa Siasa

Mabadiliko ya kisiasa huacha wasanii  katika hali ngumu ya kuamua ikiwa wakumbatie utawala uliopo au kuunga mkono wnaaodai mabadiliko.

Msanii kama kioo cha jamii huacha athari pale anapounga mkono upande mmoja dhidi ya mwengine. Na hilo humuweka katika hali ya sintofahamu hasa pale upande anaoupigia debe ukiwa haukubaliki na wengi.

Wapo walionufaika na hilo wapo waliohatarisha maisha yao, nakupelekea kuanguka kimvuto na kazi zao kutothaminika.

Uchaguzi mkuu wa rais na wabunge ulifanyika oktoba ,2010 na kuwagawanya wasanii wetu kugawanyika pande mbili .Kambi ya Chama tawala CCM licha yakuwa na bendi yao ya TOT walikuwa na wasanii wengine kama Marlow na kwa upande wa upinzani hasa Chadema walikuwa na wasanii kama MR II maarufu kama Joseph Mbilinyi  ,Mbunge wa Mbeya Mjini na Fred Maliki maarufu Mkoloni.

Wapo waliokuwa  watazamaji na wapo waliobadili upepo mwishoni kama Nakaaya Sumari yaani muhimu uelewe ya kuwa kwa njia moja au nyengine upepo wa siasa unawaathiri sana wasanii kuliko mwananchi wa kawaida.

Hayo yakijiri nyumbani hali hiyo imewakuta hata wasanii wa nje,huko Misri ambako vuguvugu la siasa la kudai mabadiliko dhidi ya rais Hosni Mubarak umewaacha wasanii wakiwa ni wahanga wa upepo wa siasa.

Ni hivi karibuni msanii maarufu wa nchi hiyo Tamer Hosny ambaye alitumia nafasi yake kuwashawishi vijana kuilinda Misri kwa kuacha maandamano na kurudia maisha ya kawaida.Amejikuta kwenye hali ngumu mara upepo wa mabadiliko ulipomvuta hadi uwanja maarufu wa Ukombozi  yaani Tahrir Square (Liberization Square) nakujikuta akipata kichapo huku akijitetea kuwa alilanguliwa na Television ya Misri nakuwa hakuwa na nia mbaya na ameshatunga nyimbo ya Mapinduzi kuashiria kuunga mkono mabadiliko.

Tamer Hosny alivyo chezea kibano

Tamer Hosny moja ya nyimbo zake

Marlow na pipi

Saturday, January 29, 2011

Sauti Ya Umma Wa Misri

Cliton on Egypt ptotest


OBAMA ON EGYPT PROTEST


Mubarak avunja baraza la Mawaziri na kutangaza Mabadiliko

Sauti Ya Amerika na Mabadiliko Misri


Waandamanaji wakionesha hasira zao kwa Utawala wa Mubarak

Ilikuwa ni Ijumaa nzito kwa kipindi cha miaka  30 cha utawala wa Hussein Mubarak(82), siku ambayo wingu la mabadiliko ya siasa ulipofunga na kusababisha mpasuko wa radi uliotingisha si tu utawala wa Misri bali na tawala nyengine duniani.

Haikuwahi Mji wa Cairo kuwa moto tangu mapinduzi ya mwaka 1952,lakini mshuko wa Ijumaa wa january 28,2011 ulithubutu kuvunja duru za usalama za nchi hiyo na kuonesha dunia kile ambacho wanakipigania yaani mabadiliko.

Imetosha, ni kauli kuu ya waandamanaji kuashiria kukata tamaa na mabadiliko ya kiuchumi,kisiasa na kijamii. Hali mbaya ya maisha kutokana na ukosefu wa ajira,gharama za maisha kupanda na uhuru wa kujieleza,rushwa na uasimu ndio vichocheo vilivyoamsha umma wa Misri na kumtaka Mubarak kuondoka madarakani.

Mwezi desemba Misri ilifanya uchaguzi wa wabunge wa duru ya pili na chama tawala cha National Democratic Party (NDP)   kujipatia ushindi mnono wa 80% na upinzani kujipatia 20%.Hata hivyo kelele za kubatilisha matokeo hayo ambayo upinzani ulisusia toka duru ya kwanza ya uchaguzi mwezi novemba linalifanya bunge hilo kuwa ni la chama kimoja bila mwakilishi toka upinzani.

Hapo jana utawala wa Marekani  ambao ni mshirika mkuu wa utawala wa Mubarak ambayo hutoa kiasi cha Dola 1.5 bilioni kila mwaka, umeitaka Misri kuheshimu uhuru wa kujieleza na kuruhusu maandamano,pamoja na kuwaacha huru waandamanaji na kuruhusu mitandao kufanya kazi huku ikiisisitiza Misri kusikiliza kilio cha Umma na kukubali mabadiliko.

Kutokana na shinikizo la ndani na nje ya nchi,Rais Mubarak ametangaza kulivunja baraza lake la Mawaziri na kuunda jipya hali yeye akiwa bado kiongozi mkuu atakae endeleza mabadiliko ya nchi katika muelekeo wa Misri Mpya.

Septemba,2011 kutakuwa na uchaguzi wa Rais wa Misri ambao kwa hali ilivyo upepo wa siasa unaelekea kuwa mbaya kwa Mubarak na chama chake.

Friday, January 28, 2011

Mganda Atumia Kigezo cha Ushoga Kudai Haki Ya Ukimbizi

Hatua kali ya sheria ya ushoga nchini Uganda kumempelekea Brenda Namigadde,mwanamama wa kiganda kuiomba serikali ya Uingereza kumfikiria kupata haki ya ukimbizi kuliko kurudishwa nchini Uganda.

Kwa mujibu wa mwanamama huyo ambaye amedai ni Msagaji na kwamba ni uvunjaji wa sheria nchini kwake kuwa na uhusiano wa jinsia moja hivyo kurejeshwa kwake kutahatarisha maisha yake.

Kwa mujibu wa sheria ya Uganda, ni marufuku kuwa na uhusiano wa mapenzi na mtu wa jinsia moja na yeyote atakae vunja sheria hukumu yake ni miaka 14 licha ya juhudi kubwa kugonga ukuta kwa baadhi ya wabunge waliofika mbali nakutaka "hukumu ya kifo" itumike.

Wiki hii nchini Uganda imeshuhudia mtetezi mkuu wa haki za mashoga David Kato  akiuawa na mtu asiyejulikana mara baada ya kuvamiwa nyumbani kwake,nakifo chake kimeibua hisia za watetezi wa haki za binadamu na wapenzi wa haki za mashoga kuhofia usalama wao.

Kwa mujibu wa hukumu ya Bi.Brenda Namigadde, wizara ya mambo ya ndani imeshindwa kujiridhisha na ushahidi alioutoa kwa kuwa hana vidhibitisho kuwa yeye ni Msagaji.Hivyo madai yake batili.

Hata hivyo Bi Breanda Namigadde amekata rufaa na kupeleka vielelezo zaidi ili kuiridhisha idara ya mambo yandani ya Uingereza ambayo imevipokea na kuanza kuvipitia.

Ikiwa ushahidi hautotesheleza vigezo kwa mujibu wa sheria ya Uingereza ,basi muhusika itampasa kufunga virago.

Umoja wa mataifa kupitia kamishna wake wa masuala ya wakimbizi Bw.Antonio Guterres amenukuliwa akizitaka mamlaka za kimataifa kuwapokea wakimbizi toka Uganda waliokimbia kutokana na maisha yao kuwa hatarini.
Chanzo:  BBC

Video ya David Kato kabla na baada ya Mauaji yake

Thursday, January 27, 2011

Mlinzi wa Hitler Bado Wamo


Rochus Misch mlinzi wa Hitler kwa muda wa miaka 5 alishuhudia
Hitler akijiua.

Zaidi ya miaka 65 tangu kwisha kwa vita ya pili ya dunia mlinzi wa mwisho wa Hitler anasema kwa hivi sasa hawezi kujibu e-mails kutokana na umri wake.

Rochus Misch,miaka 93 alishuhudia Hitler akijiua mara baada ya kuona kifaru cha jeshi la Urusi kimkaribia.Aliwahi kubadilishana uzoefu na Christopher McQuarrie,mwandishi aliyetengeneza Valkyrie filamu ya mwaka 2008 ikielezea jinsi Hitler alivyojiua.

Mcheza sinema wa Hollywood ,Tom Cruise ambaye aliigiza katika filamu hiyo hakutaka kukutana na Misch na kuliambia gazeti la Los Angeles Times kuwa"shetani ni shetani,haijalishi umri aliokuwa nao".

Amenukuliwa na gazeti la Berliner Kurier ya kwamba hawezi kujibu barua pepe anazotumiwa kutokana na umri aliokuwa nao.

Mwezi January 16 ,1945 kufuatia Ujerumani kushindwa vitani Misch na wasaidizi wa karibu wa Hitler walikimbilia Führerbunker katika jiji la Berlin. Nakujitokeza kwake mara baada ya vita, alijikuta akitiwa mikononi na Jeshi Jekundu . Aliachiwa huru mwaka 1954, na tangu wakati huo na hadi sasa Misch anaishi katika jiji la Berlin.

Kwakujua alivyokutana na Hitler na majukumu yake endelea......Hitler

Watch Valkyrie Trailer

Hitler Private resident

Wednesday, January 26, 2011

Waarabu Wataka Mabadiliko

        Tunisia yataka Ben Ali akamatwe          
Waziri wa sheria wa Tunisia amesema nchi hiyo imetoa hatia ya kimataifa ya kukamatwa kwa Rais aliyekimbia Zine al-Abidine Ben Ali na familia yake.


Lazhar Karoui Chebbi alisema Tunisia imeiomba shirika la polisi la kimataifa Interpol kumkamata Ben Ali, aliyekimbilia Saudi Arabia mapema mwezi huu kufuatia maandamano makubwa nchini humo.

Bw Chebbi alisema Bw Ben Ali ashtakiwe kwa wizi wa mali na kuhamisha patoa la taifa la fedha za kigeni.

Aliyasema hayo huku maandamano ya kuipinga serikali yakiendelea.

Chanzo: BBC

Maandamano Tunisia
Nyumba Ya Familia Ya  Rais Ben Ali  Yavamiwa


Mitandao imerahisisha sauti ya Umma


Misri kwafuka Moto Licha Vitisho Vya Serikali
kwa kuweka waandamanaji 500 kizuizini nakuua 4
 Marekani  Yaitaka Misri kuruhusu Maandamano
 

Palestina yajibu kuhusu 'nyaraka za siri'

Maafisa wa Palestina wameishutumu al-Jazeera kwa kupotosha, baada ya kutoa taarifa za siri zilizokusudia kuonyesha nchi hiyo kuwa na maridhiano makubwa na Israel.

Rais Mahmoud Abbas alisema siri hizo zimechanganya kwa makusudi misimamo ya Palestina na Israel.

Nyaraka hizo zinasema kuwa Palestina iliikubalia Israel kubaki na eneo kubwa la mashariki mwa Israel wanalomiliki kinyume cha sheria- jambo ambalo Israel imelikataa.

BBC imeshindwa kuthibitisha binafsi nyaraka hizo.

Al-Jazeera ilisema ina rekodi 16,076 za siri za mikutano, barua pepe, na mawasiliano baina ya Palestina, Israeli na viongozi wa Marekani, baina ya mwaka 2000-2010.

soma zaidi....... BBC

Kupitia Nyaraka zenyewe gonga hapa http://english.aljazeera.net/palestinepapers/

Maoni Ya Wachambuzi

Undugu Wamtoa Machozi Oprah Winfrey


Kwa muda wa miaka 25,mwanamama  Oprah Winfrey amebahatika kuwaunganisha watu mbali mbali katika kipindi chake maarufu cha Oprah show .

Lakini safari hii imekuwa kwa upande, katika hali ya kushangaza amejikuta anakutana na dada yake wa mama mmoja ambaye alichukuliwa kimalezi wakati yeye akiwa miaka 8.

Kwa kiasi fulani tukio hili litamliwaza Mama huyu kwani kwa kipindi kirefu alikuwa ana dai yakuwa ana asili ya Kizulu kutokana na vipimo vya DNA, hali wakuu wa kabila hilo lililopo nchini Afrika kusini wakikanusha kwa vizazi vyao kuchukuliwa utumwa kwenda Marekani.

Monday, January 24, 2011

Aljazeera kama Wikileaks Yatoa Waraka Wa Mazungumzo Baina Ya Israel Na Palestina

Mbowe; Nitawapa CCM shida ambayo hawataisahau


Mwenyekiti wa Chadema,Freeman Mbowe

MWENYEKITI wa Chadema, Freeman Mbowe amesema kuwa ana usongo na CCM na mwaka huu atawapa shida ambayo hawataisahau.


Mbowe alisema hayo jana wakati akizindua tawi na kukabidhi kadi zaidi ya 200 kwa wanachama wapya wa Chuko Kikuu Kishiriki cha Tumaini Tawi la Makumira , mkoani Arusha.

“Kwa kweli nina usongo na CCM, mwaka huu watapata shida sana kwa kuwa hivi karibuni tutafanya zaidi ya operesheni sangara, tutahakikisha tunapita kila kijiji kilichopo Tanzania bara na Visiwani kuwahamaisha watu juu ya dhana nzima ya ukombozi wa nchi hii” alisema Mbowe na kuongeza.

“Jamani CCM ni walaini kuliko embe bovu, pamoja na kutumia polisi na mabomu yao, risasi za moto, usalama wa taifa na rushwa zao lakini hawa tukipambana nao tunawapiga goli 10 asubuhi asubuhi tu,” alisema.

Alisema CCM wasifikiri Chadema wamebweteka na wabunge 48, madiwani wengi na halmashauri wanazoziongoza,hivi sasa ndiyo kazi ya kuchukua madaraka ya nchi imeshaanza kutokana na kuhakikisha kila pembe ya nchi inafikiwa na ujumbe wa ukombozi.

Akiwahutubia kundi la wanachuo wa chuo hicho tawi la Makumira katika Hoteli ya kitalii ya Ndoro nje kidogo ya Jiji la Ausha, alisema wasomi wa vyuo vikuu wakichukua kadi za Chadema bila ya kupiga vita ufisadi na kutetea haki za Watanzania wanyonge ni kazi bure.

“Sisi Chadema tunasema, unatakiwa uhubiri kitu ambacho unakifanya na unachokifanya ndicho unachotakiwa kukihubiri, ndio maana hata ndani ya Chadema tunapiga vita ufisadi na maovu mengine yote yanayofanywa na serikali ya CCM, hata sisi Chadema tunajisafisha wanaofanya vibaya tunawaondoa, hatuoneani aibu,”alisema Mbowe.

Aliwaasa wanavyuo hao kuwa makini na matendo yao na kuongeza kuwa yoyote hata akichakachua kadi za wananchama wa Chadema hatakuwa nafasi ndani ya chama chake.

“Jiungeni kwa wingi tukomboe nchi, kwa taarifa yenu fursa za uongozi Chadema ziko nyingi kwa wasomi kama nyie na chama hiki kinakua kwa kasi sana hapa nchini baaada ya tukio la Januari 5 baada ya serikali kuona kuwa wanaikomesha Chadema kwa kutupiga mabomu na kutuweka ndani,"alisema.

Alisema kila mkoa hivi sasa wanataka kuandamana na kupigwa risasi kama Arusha ili waingie kwenye kumbukumbu ya ukombozi wa Taifa na wameshaanza kuonekana hata jana vyombo vya habari vimeonyesha ya Dodoma na Songea. Mbowe alisema leo baada ya kutoka katika uzinduzi wa tawi hilo ataenda jimboni kwake Hai na baadaye jijini Dar es salam kwenda kupanga mikakati mizito ya kwa ajili kuimarisha chama.

Akigusia kitendo cha polisi siku ya maandamano ya Januari 5, Mbowe alisema viongozi wa Chadema walikuwa tayari kwa lolote hata kupoteza maisha kwa ajili ya kizazi kinachokuja.

“Ndugu zangu ile siku haikuwa ya mchezo, tulianza maandamano yetu pale Hoteli ya Mt. Meru na tulipofika Tangi la maji polisi walifika na bunduki za kivuta na mabomu ya mchozi wakiwa wameshakoki, tukawaambia tupigeni vifuani tuko tayari kufa kwa ajili ya Taifa” Alisema

Naye Mwenyekiti wa muda wa Tawi la Chadema chuoni hapo Mwalimu, Restituta Kayombo akielezea kuwa mwamko wa kuunda tawi chuoni hapo ilikuwa ni changamoto ya uchaguzi wa mwaka jana wakati matokeo yalipokuwa yakitangazwa na kuonyesha Chadema kuongoza katika sehemu nyingi za nchi.
Chanzo: Mwananchi

Sunday, January 23, 2011

Kula Wadudu Kuokoa Mazingira


Mifugo ikitaabika kutokana na ukame ulosabibisha kukosa lishe
na maji.

Utafiti uliofanyika toka Discover Magazine umegundua ya kuwa kutokana na tatizo la chakula duniani,ukame wa ardhi,maji na uharibifu wa mazingira ili kuokoa mazingira hatua mbadala zinapaswa kuchukuliwa ikiwamo kubadili aina ya maakuli yetu.

Utafiti umegundua ya kuwa ufugaji wa wadudu kama senene,kumbi kumbi,barare na aina za minyoo hauhitaji mradi mkubwa wa ardhi,maji, kwani upatikanaji wake hauhitaji uangalizi mkubwa kama ule wa mifugo ya ng'ombe,mbuzi ,kondoo,nguruwe ambao wanahitaji ardhi na maji ya kutosha hali inayopelekea uhaba wa ardhi na maji hivyo kusababisha ukame na uhaba wa chakula.

Ripoti ya umoja mataifa ya mwaka 2006 inasema kuwa sekta ya ufugaji huchangia 18% ya uchafuzi wa mazingira  duniani kwa kuzalisha kaboni kuliko sekta ya usafirishaji na ndio chanzo kikuu cha kusababisha ukame wa ardhi na maji.Katika utafiti huo wametahadharisha ya kuwa ifikapo mwaka 2050 uzalisha wa wanyama hao utafikia tani 465 maradufu ya takwimu ya mwaka 2000.

Katika toleo hilo umemalizia kwa kuelezea ya kuwa wadudu wanakiasi kidogo cha protini na mlo mzuri kuliko nyama kwani wanyama wana mafuta mengi ambayo ni hatari kwa afya.

Saturday, January 15, 2011

Si Risasi Bali Ni Mawe Tu Yamkimbiza Rais Wa Tunisia

Ni kisa cha kijana msomi,26 mchuuzi wa matunda katika mji wa Sidi Bouzid kuhujumiwa na polisi kwa madai ya kufanya biashara kwa njia isiyo halali na kupelekea kujitoa muhanga kwa kujiwasha moto kupinga hali ya ukosefu wa ajira na malipo madogo ya ujira.

Kujitoa muhanga kwa kijana huyo kulipelekea muamko katika mji wa Sidi Bouzid na kuamsha hisia za uchungu juu ya hali ngumu ya maisha  na ukosefu wa ajira na kupelekea umma wa Tunisia kuamua kuingia barabarani kumtaka Rais wao kujiuzulu.

Rais Zine al Abidine Ben Ali aliitawala Tunisia kidiktekta kwa miaka 23 kwa mapinduzi ya kijeshi bila kumwaga damu huku akiwaweka vizuizini wapinzani wake, kuzuia uhuru wa habari huku akishindwa kukabiliana na tatizo la ajira.

Maandamano  ya tarehe 17/12/2010 yaliandaliwa na Chama cha wafanyakazi cha Tunisia nakuchukua muda wa mwezi mmoja kwa kugharimu maisha ya watu 23 yamepelekea Rais Zine al Abidine Ben Ali kuikimbia nchi na kwenda uhamishoni Saudi Arabia .

Nchi za magharibi ambazo zilikuwa washirika wakubwa wa rais Ali zimebariki mapinduzi hayo na kuyaita hatua ya kuelekea kwenye demokrasia ya kweli huku ufaransa mtawala wa zamani wa nchi hiyo ikikataa kutoa hifadhi ya ukimbizi wa rais Ali na Mkewe.

Monday, January 10, 2011

Jicho La Dunia Na Mustakbali wa Sudan

               Bashir kuchukua madeni yote ya Sudan Kusini

Rais wa Sudan, Omar Hassan al-Bashir amesema kuwa yuko tayari kuchukua madeni yote ya nchi hiyo iwapo eneo la Sudan Kusini litajitangazia uhuru wake baada ya kura ya maoni. Taarifa hiyo imetolewa leo na rais wa zamani wa Marekani, Jimmy Carter alipozungumza na kituo cha televisheni cha CNN.

Iwapo ahadi hiyo itathibitishwa, itakuwa ni ishara muhimu ya mapatano kutoka kwa Rais Bashir na itainua mzigo mkubwa wa fedha za serikali katika eneo la Kusini katika siku za mwanzo za uhuru wake unaotarajiwa. Bwana Carter amesema kuwa amezungumza na Rais Bashir ambaye amesema deni lote lazima lipelekwe Sudan Kaskazini na siyo Kusini.

Wakati hayo yakijiri Wasudan Kusini wameingia katika siku ya pili ya kupiga kura ya maoni ya kuamua iwapo wajitenge na Kaskazini na kuwa taifa huru, zoezi litakaloenda hadi tarehe 15 ya mwezi huu wa Januari. Aidha, kwa upande mwingine, watu zaidi ya 20 wameuawa katika mapigano ya Wasudan wenye asili ya Kiarabu wa kabila la Misseria na jamii ya Ngok Dinka katika eneo lenye mzozo la Abyei.
Chanzo: Dw

Sudan Taifa Kubwa kuliko yote Afrika linaelekea kugawanyika pande mbili kutokana na kura ya maoni inayoendelea Sudan ya Kusini .Angalia video upate picha ni wapi Sudan inaelekea


Gharama za Maisha na Ajira Ni Hatari Kwa watawala

Serikali nyingi zimejikuta katika wakati mgumu kutimiza ahadi kwa wananchi wao hasa masuala mazima ya kupanda gharama za maisha na ajira kwa vijana hasa wale wanaomaliza masomo yao ya elimu ya juu.Kupanda kwa gharama za maisha na ajira kwa vijana imekuwa ni jambo linahatarisha uwepo wa serikali.


Ukiyatizama masuala haya kwa makini utagundua kunamguso kwa kila jamii toka pande zote za dunia ila hutofautiana njia zakuyatatua.

Ninachotaka kufungua macho kwa serikali yetu ya Tanzania ni kutafuta njia mbadala za kujiwezesha kujikwamua toka dimbwi zito la umaskini na kusababisha sauti ya mnyonge kuchoka kuvumilia kuona wakubwa wakiji nafasi .

Inapasa kubadilishana uzoefu toka kwa marafiki zetu wa kimataifa ili kufikia lengo la kumkwamua mnyonge ,hebu  rudisha kumbukumbu za uchaguzi wa mawaka 2010 utagundua ni kutokana na hasira za wananchi ndiyo maana vyama vya upinzani vikapata viti vingi bungeni.

Inasemekana kwa matokeo ya uchaguzi mkuu CCM imeathirika hasa suala zima la posho toka bilioni 1 kwa mwezi hadi milioni 800 na kupelekea chama hicho kuchukua hatua za kurekebisha matumizi ya posho hiyo kwa kufuta posho kwa baadhi ya taasisi zake na watendaji kwenye chama.

Hapa tunapata picha ya kuwa CCM isipokuwa makini 2015 mambo yanaweza kubadilika zaidi ikiwa hatua madhubuti ya kurekebisha maisha ya mtanzania hazitachukuliwa.

Nchi kama ya  Falme ZA Kiarabu(UAE) imetunga sheria kwa ajili ya kupambana na tatizo la ajira, wakati nchi nyengine kama Algeria na Tunisia  hali imekuwa mbaya kwa vijana kuingia mitaani kulazimisha serikali zao kuangalia kupanda kwa gharama za maisha na ukosefu wa ajira.


Anger in Algeria sparks fresh riots
Uploaded by euronews-en. - Up-to-the minute news videos.

Sunday, January 9, 2011

Maaskofu Wamng'oa Naibu Meya Arusha

SIKU moja baada ya Maaskofu wa makanisa ya Kikristo mkoani Arusha kutangaza kutomtambua Meya wa Jiji la Arisha, Naibu Meya wa Jiji hilo, Michael Kivuyo (TLP), ametangaza kujiuzuru wadhifa huo.Akitangaza kujiuzulu wadhifa huo, Kivuyo alisema hawezi kuwasaliti wananchi wa Arusha kwa kuongoza sehemu iliyomwaga damu za watu.


Juzi maaskofu wa makanisa ya Kikristo mkoani Arusha, walitoa tamko la pamoja la kutomtambua Meya wa Jiji la Arusha aliyeteuliwa na CCM na kuweka bayana kwamba hawatampa ushirikiano katika uongozi wake.

Walitoa tamko hilowakati wakilaani hatua ya polisi mkoani Arusha, kutumia nguvu kupita kiasi kuvunja maandamano ya amani ya Chadema na hivyo kusababisha vifo vya watu watatu na kujeruhi wengine zaidi ya 20.
Akisoma tamko la umoja wa viongozi wa dini ya kikristo mkoani Arusha, Askofu Mkuu wa Kanisa Katoliki, Jimbo Kuu la Arusha, Josephat Lebulu alisema Jeshi la Polisi ndilo lilikuwa chanzo cha vurugu hizo.

Tamko la maaskofu hao lilitolewa siku moja tu tangu Serikali kupitia kwa Waziri wa Mambo ya Ndani, Shamsi Vuai Nahodha atoe tamko kwamba vurugu zilizotokea Arusha ni tatizo la kisiasa ambalo pia litapaswa kushughulikiwa kisiasa.

Akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari, akiwa na wajumbe wa Secretarieti ya chama chake cha TLP mkoani Aruda ya jana asubuhi, Kivuyo alisema anaungana na Watanzania wengine kulaani polisi kutumia nguvu kupita kiasi kutawanya maandamano ya amani ya Chadema.

"Mimi kama Naibu Meya ambaye nilichaguliwa Desemba 18, mwaka jana natangaza rasmi kujiuzuru kwani siwezi kuwasaliti wananchi wa Arusha kwa kuitumikia nafasi hii....kwani ni ukweli uchaguzi haukuwa halali," alisema Kivuyo.

Hili ni pigo la pili kwa CCM baada ya Diwani wake wa Kata ya Sombetini, Alfonce Mawazo kutangaza kujiondoa katika chama chake Jumatano wiki hii na kujiunga na Chadema akidai kuwa amechoshwa na ukatili wa CCM.

Mawazo ambaye alihamia CCM mapema mwaka juzi akitokea TLP akiwa diwani wa kata hiyo, alisema kwa muda mrefu amekuwa akiunga mkono sera za Chadema na sera binafsi za aliyekuwa mgombea wa urais wa chama hicho, Dk Willibroad Slaa.

"Naomba niwaeleze wazi kuwa hata katika Uchaguzi Mkuu ingawa mimi nilikuwa mgombea wa udiwani wa CCM, nilimchagua Dk Slaa kwa nafasi ya urais," alisema Mawazo katika mkutano wa hadhara uliohutubiwa na Dk Slaa.

Diwani Kivuyo alieleza kuwa, katika mazingira yaliyopo sasa, Uchaguzi wa Meya Arusha unapaswa kurudiwa ili taratibu zifuatwe na amani irejee katika mji wa Arusha.

"Mimi binafsi kabla ya maandamano ya Chadema, nilikwenda kuonana na Mkuu wa Mkoa Arusha, Isdore Shirima nikamuomba aitishe kikao cha vyama vyote na tuzungumze ili kurejesha amani, lakini hakutekeleza," alisema Kivuyo.

Kivuyo ambaye ni Diwani wa Kata ya Sokoni One, alisema anaungana na Watanzania wengine kulaani mauaji ya kinyama ya polisi na kuwapa pole majeruhi wote na wafiwa.

Jumatano wiki hii vurugu kubwa ziliibuka mkoani Arusha na kusababisha polisi kuua watu watatu na wengine zaidi ya 20 kujeruhiwa wakati wakiwatawanya watu walioshiriki maandamano yaliyoandaliwa na Chadema.

Risasi za moto na mabomu ya machozi vilitumika wakati polisi wakizuia maandamano hayo kutekeleza amri ya Mkuu wa Jeshi hilo, Ispekta Jenerali Saidi Mwema.

IGP Mwema alitoa amri ya kupiga marufuku maandamano hyo jioni ya kuelekea siku iliyopangwa kufanyakia kwa maelezo kuwa taarifa za kiintelijensia zimebaini kwamba kungekuwa na vurugu.

Kufuatia tukio hilo viongozi kadhaa wa Chadema akiwamo Mwenyekiti wake, Freeman Mbowe, Katibu Mkuu wa chama hicho, Dk Wilbroad Slaa na wabunge kadhaa walikamatwa na kufikishwa mahakamani kwa madai ya kukusanyika bila ya kibali.

Katika hatua nyingine, TLP mkoa wa Arusha kimemtaka IGP, Said Mwema na Waziri wa Mambo ya Ndani, Shamsi Vuai Nahodha kujiuzuru kutokana na kuagiza polisi kuuwa Raia kwa risasi na kujeruhi wengine.

Mwenyekiti wa TLP mkoa wa Arusha, Leonard Makanzo alisema jana kuwa kitendo cha polisi kuvunja kwa nguvu maandamano ya Chadema na kuwauawa kwa risasi watu watatu na wengine zaidi ya 31 kujeruhiwa hakikubaliki.

"Tunaomba wajiuzuru nafasi zao kwani wameshindwa kufanya kazi ya kulinda raia na mali zao badala yake wanafanya kazi ya kufanya vurugu na kuuwa raia kwa kuwapiga risas," alisema Makazo.

Alisema chama hicho kimeridhia Diwani wake, Kivuyo kujiuzuru nafasi ya Naibu Meya na kutaka uchaguzi urudiwa nakufanyika katika mazingira ya haki , amani huku taratibu kidemokrasia zikifuatwa.

Uchaguzi wa Meya Arusha uliingia dosari baada ya kufanyika bila ya kuhusisaha madiwani wa Chadema, hali ambayo ilisabisha mji wa Arusha kuchafuka kwa vurugu na Mbunge wa jimbo la Arusha Mjini, Godbles Lema kukamatwa na polisi, kupigwa na kukimbizwa hospitali baada ya kuishiwa nguvu.
Chanzo: Mwananchi

Thursday, January 6, 2011

Mchezo wa Argentina - Benki Zetu Ziwe Macho

Licha ya kuwa na kamera na viashiria sauti hilo halikuweza kuwazuia majambazi kutojichotea zaidi ya Dola milioni 6 katika tawi la Belgrano la benki ya Provincia Bank ,Argentina.

Majambazi hao walikodisha jengo ambalo limeambatana pamoja na benki hiyo,na ndipo walipotumia nyenzo mbali mbali za ujenzi na kufanikiwa kupasua ndani kwa ndani hadi kufikia chumba cha kuhifadhi fedha.
Ili chukua muda wa miezi 6 kwa majambazi hao kufanikisha zoezi hilo lilitokelezeka siku ya mkesha wa mwaka mpya.
Habari zadi............Argentina

Misri yaitega CECAFA

BARAZA la Vyama vya Soka kwa Nchi za Afrika Mashariki na Kati (CECAFA), sasa linapita katika kipindi kigumu baada ya Misri kusema itajisikia raha kama litaanzishwa Shirikisho la Soka kwa Nchi za Bonde la Mto Nile.

Kauli hiyo ya Misri ni nyepesi, lakini yenye uzito mkubwa kwani inaweza kupunguza msisimko wa mashindano ya CECAFA na hata kuyaua kabisa na badala yake yale ya nchi za Bonde la Mto Nile kuwa yapo juu, hasa katika suala la zawadi.

Juzi Chama cha Soka cha Misri (EFA) kilitangaza zawadi ya zaidi ya Sh milioni 200 kwa bingwa wa michuano ya soka kwa nchi za Bonde la Mto Nile iliyoanza jana mjini hapa ikishirikisha nchi saba.
Zawadi hiyo ni zaidi ya mara tano ya ile ambayo Tanzania Bara 'Kilimanjaro Stars' ilichukua baada ya kuibuka bingwa wa michuano ya Chalenji mwezi uliopita katika mashindano yaliyofanyika Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, ambapo Stars ilitwaa dola za Marekani 30,000 ambazo ni karibu Sh milioni 43 za Tanzania.

Kutokana na mwitikio mzuri wa nchi zinazoshiriki michuano ya Mto Nile mwaka huu, Misri imesema ipo katika mazungumzo na nchi ambazo bonde hilo lipo, ili kuzishawishi lianzishwe shirikisho hilo ambalo Misri inaamini litakuwa kitovu cha vipaji vya soka Afrika na duniani kwa ujumla.

Rais wa EFA, Samir Zahir alisema juzi kuwa kama nchi zote zitakubaliana kuanzisha shirikisho hilo itakuwa hatua moja kubwa ambayo imepigwa kwa maendeleo ya soka Afrika
Lakini EFA inaona ugumu ulio mbele juu ya kuanzishwa kwa shirikisho hilo kwa vile baadhi ya nchi tayari zipo katika vyama mbalimbali vinavyosimamia soka kwa kanda zao.

Alisema zaidi ya nusu ya nchi zinazoshiriki mashindano hayo ya Bonde la Mto Nile ni wanachama wa Baraza la Vyama vya Soka Afrika Mashariki na Kati (CECAFA), ukiacha Misri na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), ambayo ni mwalikwa katika michuano hiyo.

Nchi zinazoshiriki michuano hiyo ambazo ni wanachama wa CECAFA ni Tanzania, Kenya, Uganda, Sudan na Burundi na zimekuwa zikishiriki mashindano yanayoandaliwa na baraza hilo karibu kila mwaka.

"Tumepeana changamoto ya namna bora ya kuanzisha shirikisho letu, uwezo wa kufanya hivyo tunao maana dhamira yetu ni kuendeleza soka," alisema.

Nchi nyingine wanachama wa CECAFA ambazo hazijashiriki michuano ya Mto Nile ni Ethiopia, Eritrea, Djibouti, Rwanda na Somalia.

Misri imegharamia usafiri wa kuja Misri na kurudi nyumbani kwa kila timu pamoja na posho za wachezaji na waamuzi, zawadi mbalimbali kwa washindi.

Bingwa wa michuano hiyo atazawadiwa zaidi ya Sh milioni 200 za Tanzania. Pia Rais huyo wa EFA, alieleza kuwa michuano yao ni maalumu kuhamasisha soka na haihusiani na masuala ya kisiasa na kwamba mambo yanayohusiana na siasa ni jukumu la wahusika wenyewe.

"Kwangu mimi ukiniuliza michuano ya soka kwa nchi za Bonde la Mto Nile ina madhumuni gani, nitakwambia ni kuinua soka. Hilo ndilo jibu langu na ndicho ninachokiamini," alisema.

Alieleza kuwa mwaka huu mashindano hayo yamefanyika Misri, hivyo nafasi ipo wazi kwa nchi nyingine ambayo itakuwa tayari kuyaandaa na kwamba Misri itatoa msaada wa karibu zaidi ili kuyafanikisha.
Chanzo: HabariLeo

Wakati huohuo,ufunguzi wa michuano ya soka kwa nchi za bonde la mto mto Nile yaliyofunguliwa jana,kati ya wenyeji Misri na Tanzania yalikuwa kama hivi.

Monday, January 3, 2011

Tunaelekea Kula Kwa Kushiba Moshi

Muelekeo wa dunia kwa sasa kila mamlaka inalia hali,ukweli hakuna nafuu ila tutarajie kuumizana ili kufikia malengo ya kiutawala na uchumi.

Mwaka 2010 ulikuwa ni mwaka wa serikali za nchi za ulaya kufunga mkanda kwa kubana matumizi ili kukabiliana na anguko la uchumi, msukumo uliopelekea kufanya hivyo ni kuweza kutunisha mfuko wa kulipa madeni yanayo yakabili mataifa hayo.

Sijui kama tushapata picha kuwa mwaka huu mpya 2011 mlango unaelekea kufungwa na nchi zetu changa haja zetu hatuziwezi tunategemea muhisani mwenye funguo.

Kwa taarifa , wahisani wanahaha kuweka serikali zao sawa maana wanajua wananchi waliowaweka wasipotimiziwa haja zao basi kura itakuwa fimbo.

Kesho wakaazi wa Uingereza  wataanza kukamuliwa kwa kulipa kodi ya ongezeko la thamani(VAT) toka 17% hadi 20% ,athari ya ongezeko la kodi ni kupungua mauzo ya bidhaa sokoni nakutokana na hilo Makampuni yatabidi kupunguza wafanyakazi na kuathiri soko la ajira.

 India inakabiliwa na ongezeko la bei ya vyakula,nchi ambayo soko kubwa la mazao yake lipo Mashariki ya kati . Kwa hali hiyo bei za vyakula kwa nchi za Mashariki ya kati zinatarajiwa kupanda na kupelekea wakaazi wake ambao wengi wao ni wageni toka nchi za nje kuzama zaidi mfukoni .

Hatua muhimu ambazo serikali inatakiwa kuzichukua kabla "hatujaelekea kula kwa kushiba moshi" ni kubana matumizi yake hasa posho za vikao na misafara ya wakubwa.Mfano mzuri ni matukio ya hivi karibuni kwa Waziri Mkuu(Mtoto wa mkulima)  kukataa gari la kifahari na kitendo cha waziri wa fedha Mustafa Mkullo kufanya ubadhirifu kwa kukodi ndege na kuagiza kupelekewa gari lake Dodoma .

Kilimo kwanza lazima kutiliwa mkazo wa hali ya juu kwani ongezeko la bei ya chakula linahatarisha amani ya wananchi.Mara nyingi tunapoona ndiyo tunapopata fundisho, siku za hivi karibuni nchi ya  Tunisia imejikuta ikikabiliwa na maandamano kutokana na halingumu ya maisha iliyotokana na ongezeko la watu  kukosa ajira.
Nathubutu kusema hivyo kutokana na kuwa "njaa ikiingia mlangoni ,amani hutokea dirishani" uvumilivu una kiasi chake nacho nikupatiwa ufumbuzi ili nafuu ya maisha ipatikane.

Serikali inatakiwa kujipanga vizuri ilikujikwamua kiuchumi bila kutarajia huruma za wahisani kufanikisha bajeti zetu, ni kwa kutumia vyema raslimali zetu kama bandari,viwanja vya ndege, vivutio vya utalii ,ardhi yenye rutuba,madini na gesi.

Hayo yote yakiwezekana Tanzania haitakuwa tena ikitembeza kikapu kwa wahisani zetu, kwani dunia ya sasa "Tunaelekea kula kwa kushiba Moshi" .



Sunday, January 2, 2011

Matokeo Ya Ligi kuu Ya Uingereza Wikiendi Hii

Sat 01/01/11 West Bromwich 1 - 2 Manchester United
Liverpool 2 - 1 Bolton Wanderers
Manchester City 1 - 0 Blackpool
Stoke City 2 - 0 Everton 
Sunderland 3 - 0 Blackburn Rovers 
Tottenham Hotspur 1 - 0 Fulham
West Ham United 2 - 0 Wolverhampton
Birmingham City 0 - 3 Arsenal

Sun 02/01/11 Chelsea 3 - 3 Aston Villa

Msimamo wa kila timu baada ya mechi 5 za mwisho
1 Manchester United 19 11 8 0 41 18 +23 41 W D W W W
2 Manchester City 21 12 5 4 33 16 +17 41 W W W L W
3 Arsenal 20 12 3 5 42 22 +20 39 W D W L W
4 Tottenham Hotspur 20 10 6 4 30 23 +7 36 W W W D D
5 Chelsea 20 10 5 5 36 18 +18 35 D W L D D
6 Sunderland 21 7 9 5 24 22 +2 30 W L L W D
7 Bolton Wanderers 21 7 8 6 33 28 +5 29 L L W L W
8 Stoke City 20 8 3 9 25 24 +1 27 W L W L D
9 Liverpool 19 7 4 8 23 24 -1 25 W L L W L
10 Newcastle United 20 7 4 9 29 31 -2 25 W L L W L
11 Blackpool 18 7 4 7 26 30 -4 25 L W W D W
12 Blackburn Rovers 21 7 4 10 26 34 -8 25 L W L D L
13 Everton 20 4 10 6 21 24 -3 22 L D W D D
14 West Bromwich … 20 6 4 10 26 36 -10 22 L L L L W
15 Aston Villa 20 5 6 9 23 37 -14 21 D L L W L
16 West Ham United 21 4 8 9 22 33 -11 20 W D W D L
17 Wigan Athletic 20 4 8 8 17 32 -15 20 L D W D D
18 Fulham 20 3 10 7 19 24 -5 19 L W L D L
19 Birmingham City 19 3 10 6 18 24 -6 19 L D L D D
20 Wolverhampton … 20 5 3 12 20 34 -14 18 L W L W L





Ubalozi Wagoma Kutoa Viza Kwa Tajiri Wa Chelsea-Roman Abramovich

Tajiri wa klabu ya Chelsea ,Roman Abramovich jitihada zake
 za kuwaombea viza vijana wa Kitanzania zimegonga ukuta.
Roman Abramovich, the owner of Chelsea football club, attempted to reward African porters who helped him on his failed attempt to climb Mount Kilimajaro by flying them to London to watch a Chelsea game only to be thwarted by red tape.
Roman Abramovich,kushoto akiwa na Mpenzi wake
Daria Zukhova,walifanya ziara ya kupanda mlima Kilimanjaro
mwaka jana.
Mwezi septemba mwaka jana,Abramovich na ujumbe wake wa watu 6 ulifanya ziara ya Tanzania kwa ajilii ya kupanda Mlima Kilimanjaro.

Mlima Kilimanjaro wenye urefu wa 19,330ft ndio mlima mrefu kuliko yote Afrika, kwenye kuupanda mlima huo Abramovich alifikia urefu wa  15,100ft nakushindwa kupumua kutokana hali ya hewa kuwa nzito hivyo kupatiwa msaada na Wapagazi nakumuwezesha kufika chini salama.

Kufuatia kitendo cha kiutu cha wapagazi hao,Abramovich aliwaahidi kuwalipa hisani kwa kuwapa mualiko kwenda London kuangalia timu ya Chelsea itakapokuwa uwanjani kwenye ligi kuu ya Uingereza.

Lakini jitihada zake hazikufanikiwa kufuatia Ubalozi wa Uingereza kuwakatalia vijana hao Viza mara mbili kwa shaka ya kutoroka pindi watakapo kuwa nchini Uingereza.

Licha ya timu ya Chelsea kutoa mualiko na kutayarisha mazingira ya ujio wao kwa kuandaa usafiri wa kwenda na kurudi,malazi na vyakula,juhudi zote hazikuweza kubadilisha msimamo wa Ubalozi wa Uingereza nchini Tanzania kubadili msimamo wake.
Chanzo: Telegraph

Wakati huo huo Chelsea imepokwa ushindi Dakika ya lala salama
Na matokeo ya kawa Chelsea 3 Vs Aston Villa 3

Saturday, January 1, 2011

Kikwete: Ni mwaka wa Katiba mpya


Rais Jakaya Kikwete

Rais Jakaya Kikwete ametangaza kuanza mchakato wa kuandikwa kwa Katiba Mpya. Katika salamu zake za mwaka mpya kwa Taifa jana, Rais Kikwete alisema "...nimeamua kuunda Tume maalum ya Katiba, yaani Constitutional Review Commission. Tume hiyo itakayoongozwa na mwanasheria aliyebobea, itakuwa na wajumbe wanaowakilisha makundi mbalimbali katika jamii yetu kutoka pande zetu mbili za Muungano".

Alisema jukumu la msingi la Tume hiyo litakuwa ni kuongoza na kuratibu mchakato utakaowashirikisha wananchi wote vikiwemo vyama vya siasa, wanasiasa, wafanyabiashara, asasi za kiraia, mashirika ya dini, wanataaluma na makundi mbalimbali ya watu wote, katika kutoa maoni "wayatakayo kuhusu Katiba ya nchi yao".
Kwa mujibu wa Rais Kikwete, baada ya kukamilisha kukusanya maoni, Tume itatoa mapendekezo yake yatakayofikishwa kwenye vyombo stahiki vya Kikatiba kwa kufanyiwa maamuzi. "Baada ya makubaliano kufikiwa, taifa letu litapata Katiba mpya kwa siku itakayoamuliwa ianze kutumika,"alisema Rais Kikwete.

Rais alisema lengo la kuandikwa kwa Katiba mpya ni kuiwezesha nchi kuwa na Katiba inayoendana na taifa lenye umri wa nusu karne na kwamba mchakato huo ni sehemu ya maadhimisho ya miaka 50 ya Uhuru wa Tanzania Bara na kwamba Katiba inayokusudiwa ni ile itakayolipeleka taifa miaka 50 ijayo kwa salama, amani, umoja na kuwepo maendeleo makubwa zaidi.

"La nne ambalo tulilokubaliana kufanya ni kuanzisha mchakato wa kuitazama upya Katiba ya Nchi yetu kwa lengo la kuihuisha ili hatimaye Katiba yetu ya sasa tuliyoachiwa na waasisi wa taifa letu, imeifanyia nchi yetu mambo mengi mazuri na kuifikisha Tanzania na Watanzania hapa tulipo," alisema KIkwete na kuongeza:

".....mwaka 2011, nchi yetu inatimiza miaka 50 ya Uhuru wa Tanzania Bara, miaka 47 ya Mapinduzi matukufu ya Zanzibar na miaka 47 ya Muungano wa nchi zetu mbili. Yapo mabadiliko mengi yaliyotokea katika nyanja mbalimbali za maisha ya nchi yetu na watu wake katika kipindi hiki. Kwa ajili hiyo ni vyema kuwa na Katiba inayoendana na mabadiliko na matakwa na hali ya sasa".

Alisema ana matumaini kwamba mchakato huo utaendeshwa kwa amani na utulivu kama ilivyo sifa ya Tanzania na mazoea yetu ya kujadiliana bila kugombana.

"Wananchi watapewa fursa ya kutosha ya kutoa maoni yao kwa uhuru na pawepo kuvumiliana kwa hali ya juu pale watu wanapotufautiana kwa mawazo,"alisema Rais Kikwete na kuonya kuwa pasiwepo kutukanana, kudharauliana, kushutumiana, kubezana, kuzomeana wala kushinikizana.

"Naomba washiriki waongozwe kwa hoja badala ya jazba. Tukiwa na jazba, hasira na kushinikizana kamwe hatutaweza kutengeneza jambo jema. Na inapohusu Katiba ya Nchi itakuwa hasara tupu. Haitakuwa endelevu na kulazimika kufanyiwa marekebisho mengi mwanzoni tu baada ya kutungwa,"alisema.

Alitoa wito kwa Watanzania wenye maoni yao kujiandaa kushiriki kwa ukamilifu katika mchakato huo na kutoa maoni ambayo yatawezesha nchi kuwa na Katiba itakayokidhi matakwa ya sasa na ya miaka 50 ijayo.

Tangazo la Rais Kikwete kuhusu kuanza kwa mchakato wa kuandikwa kwa upya kwa Katiba, ni faraja kwa makundi mbalimbali ya kijamii ambayo tangu kumalizika kwa uchaguzi mkuu, Oktoba 31, 2010 yamekuwa yakitoa wito wa kaundikwa kwa Katiba mpya.

Moto wa kudai katiba mpya, uliwashwa na Chadema Novemba mwaka jana, baada ya kutangaza kutotambua kura zilizomweka madarakani Rais Kikwete. Kutokana na hali hiyo, chama hicho kilianza mchakato wa kushikiza kuundwa kwa katiba mpya kwa kususia hotuba ya Rais Kikwete wakati wa akizindua Bunge la Kumi.

Pia wabunge pamoja na viongozi wa chama hicho walisusia sherehe za kuapishwa kwa Rais. Katika kuendeleza madai hayo, hizi karibuni mbunge wa Jimbo la Ubungo kupitia Chadema John Mnyika aliwasilisha hoja binafsi kwenye Ofisi za Bunge, hoja iliyokuwa na lengo la kudai katiba mpya.

Hivi karibuni pia, CUF walifanya maandamano ya kuwasilisha rasimu ya katiba mpya kwa waziri wa Katiba na Sheria. Pia viongozi mbalimbali wastaafu, walipo madarakani wamekuwa wakieleza umuhimu wa kuwa na Katiba mpya.

Miongoni mwa waliojitokeza adharani na kuunga mkono uwepo wa katiba mpya ni pamoja na Rais Mstaafu, Benjamin Mkapa, mawaziri wakuu wa zamani, Joseph Warioba na Frederick Sumaye , Jaji Mkuu Mstaafu na Agostino Ramadhani, Mwanasheria Mkuu wa Zanzibar, Jaji Omar Makungu pamoja na waziri Mkuu, Mizengo Pinda ambaye aliahidi kumshauri Rais juu ya suala la kuundwa kwa Katiba mpya.

Madai ya Katiba mpya pia yamewahi kutolewa na Msajili wa Vyama vya Siasa, John Tendwa ambaye alisema bayana kuwa katiba mpya iandikwe mapema kabla ya mambo kuwa mabaya, akitoa mfano wa mapungufu ya katiba ya sasa kuwa ni rais kupewa madaraka makubwa.

Lakini akiwa Ikulu kwenye hafla ya kuapishwa Jaji Mkuu Mpya, Mohamed Othman Chande, Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG) Frederick Werema, alisema kuwa haona haja ya kuandikwa katiba mpya badala yake katiba iliyopo, iwekewe viraka.

“Kuandika Katiba mpya hapana, lakini kufanya marekebisho kwa kuondoa au kuongeza mambo fulani kwenye katiba, ruksa,” alisema Jaji Werema.

Wakati huohuo, Rais Kikwete ameutangaza mwaka 2011 kuwa mwaka wa maadhsimisho ya miaka 50 ya Uhuru ambayo kilele chake kitakuwa tarehe 9 Desemba, 2011 ambapo kutafanyika sherehe kubwa na za aina yake nchi nzima na wananchi kushirikishwa kikamilifu.

"Kwa kutambua umuhimu wa aina yake wa maadhimisho ya mwaka huu ya siku ya Uhuru wa Tanzania Bara tarehe 9 Desemba, 2011, tumekubaliana na viongozi wenzangu serikalini kuwa tusherehekee siku hiyo kwa uzito unaostahili," alisema.

Kadhalika Rais alisema jambo jingine ni kufanyika kwa tathmini ya kina ya mafanikio tuliyoyapata na tahmini hizo kuandikwa katika vitabu ili kuhifadhi kumbukumbu hizo muhimu kwa vizazi vijavyo.

"Vitabu na nyaraka hizo vitakuwa kumbukumbu zenye manufaa makubwa kwa wenzetu watakaokuwepo mwaka 2061 wakati wa kusherehekea miaka 100 ya Uhuru wa Tanzania Bara" alisema na kuongeza kuwa pia yatafanyika maonyesho maalum katika Uwanja wa Maonyesho wa Julius Nyerere, Dar es Salaam na kote mikoani kwenye viwanja vya maonyesho, kuelezea mafanikio yaliyopatikana katika nyanja mbalimbali katika miaka 50 tangu Uhuru wa Tanzania Bara.
Angalia video................. JK 2011

Wauwa Katika Mkesha wa Mwaka Mpya

Alexandria,Misri
Watu 21 wauwa wakitoka kwenye misa ya mwaka mpya


Abuja,Nigeria
Kumetokea mlipuko mkubwa katika eneo lenye mkusanyiko mkubwa wa watu
Walikuwa wapo kwenye Mkesha wa Mwaka Mpya
Takribani watu 4 wauawa na 13 kujeruhiwa kwa mujibu wa maofisa wa polisi
wakati TV ya Taifa imetoa idadi ya waliouwa ni watu 30.
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...