Mtazamohalisi

Friday, December 10, 2010

AU Yaisimamisha Ivory Coast Uanachama

Shinikizo la kumtaka Rais Laurent Gbagbo wa Cote d'Ivoire kujiuzulu kufuatia mabishano yaliyozuka katika uchaguzi wa rais nchini humo limepamba moto hii leo, baada ya viongozi duniani kumzuia na wapinzani wake wa ndani kutaka jeshi liwatii.


Baada ya Umoja wa Afrika kuisimamisha Cote d'Ivoire uwanachama na Marekani kuonya kuiwekea vikwazo, utawala ulioanzishwa na mpinzani wake, Alassane Ouattara, umelitaka jeshi kumtambua yeye kama mkuu wa nchi hiyo. Taarifa iliyotolewa na serikali ya Ouattara imevitaka vikosi vya usalama na jeshi kuendesha shughuli zake kwa kufuata maagizo ya Ouattara, ambaye ni amiri jeshi mkuu.

Wito huo unazidi katika jitihada za kumbana Gbagbo ambaye anakabiliwa na hatua ya kutengwa huku kukiwa na shinikizo la kumtaka aachie madaraka kutoka kwa nchi zenye nguvu duniani, likiwemo Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, Umoja wa Afrika na wadau wengine muhimu wa kikanda. Mapema serikali ya Ouattara ilisema kutakuwa na utawala wenye ufanisi nchini Cote d'Ivoire, lakini Gbagbo bado hajalizungumzia suala hilo na wananchi wa Cote d'Ivoire wanasubiri kwa hamu hatua yake itakayofuata.
Chanzo: Dw

No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...