Mtazamohalisi

Saturday, January 1, 2011

Kikwete: Ni mwaka wa Katiba mpya


Rais Jakaya Kikwete

Rais Jakaya Kikwete ametangaza kuanza mchakato wa kuandikwa kwa Katiba Mpya. Katika salamu zake za mwaka mpya kwa Taifa jana, Rais Kikwete alisema "...nimeamua kuunda Tume maalum ya Katiba, yaani Constitutional Review Commission. Tume hiyo itakayoongozwa na mwanasheria aliyebobea, itakuwa na wajumbe wanaowakilisha makundi mbalimbali katika jamii yetu kutoka pande zetu mbili za Muungano".

Alisema jukumu la msingi la Tume hiyo litakuwa ni kuongoza na kuratibu mchakato utakaowashirikisha wananchi wote vikiwemo vyama vya siasa, wanasiasa, wafanyabiashara, asasi za kiraia, mashirika ya dini, wanataaluma na makundi mbalimbali ya watu wote, katika kutoa maoni "wayatakayo kuhusu Katiba ya nchi yao".
Kwa mujibu wa Rais Kikwete, baada ya kukamilisha kukusanya maoni, Tume itatoa mapendekezo yake yatakayofikishwa kwenye vyombo stahiki vya Kikatiba kwa kufanyiwa maamuzi. "Baada ya makubaliano kufikiwa, taifa letu litapata Katiba mpya kwa siku itakayoamuliwa ianze kutumika,"alisema Rais Kikwete.

Rais alisema lengo la kuandikwa kwa Katiba mpya ni kuiwezesha nchi kuwa na Katiba inayoendana na taifa lenye umri wa nusu karne na kwamba mchakato huo ni sehemu ya maadhimisho ya miaka 50 ya Uhuru wa Tanzania Bara na kwamba Katiba inayokusudiwa ni ile itakayolipeleka taifa miaka 50 ijayo kwa salama, amani, umoja na kuwepo maendeleo makubwa zaidi.

"La nne ambalo tulilokubaliana kufanya ni kuanzisha mchakato wa kuitazama upya Katiba ya Nchi yetu kwa lengo la kuihuisha ili hatimaye Katiba yetu ya sasa tuliyoachiwa na waasisi wa taifa letu, imeifanyia nchi yetu mambo mengi mazuri na kuifikisha Tanzania na Watanzania hapa tulipo," alisema KIkwete na kuongeza:

".....mwaka 2011, nchi yetu inatimiza miaka 50 ya Uhuru wa Tanzania Bara, miaka 47 ya Mapinduzi matukufu ya Zanzibar na miaka 47 ya Muungano wa nchi zetu mbili. Yapo mabadiliko mengi yaliyotokea katika nyanja mbalimbali za maisha ya nchi yetu na watu wake katika kipindi hiki. Kwa ajili hiyo ni vyema kuwa na Katiba inayoendana na mabadiliko na matakwa na hali ya sasa".

Alisema ana matumaini kwamba mchakato huo utaendeshwa kwa amani na utulivu kama ilivyo sifa ya Tanzania na mazoea yetu ya kujadiliana bila kugombana.

"Wananchi watapewa fursa ya kutosha ya kutoa maoni yao kwa uhuru na pawepo kuvumiliana kwa hali ya juu pale watu wanapotufautiana kwa mawazo,"alisema Rais Kikwete na kuonya kuwa pasiwepo kutukanana, kudharauliana, kushutumiana, kubezana, kuzomeana wala kushinikizana.

"Naomba washiriki waongozwe kwa hoja badala ya jazba. Tukiwa na jazba, hasira na kushinikizana kamwe hatutaweza kutengeneza jambo jema. Na inapohusu Katiba ya Nchi itakuwa hasara tupu. Haitakuwa endelevu na kulazimika kufanyiwa marekebisho mengi mwanzoni tu baada ya kutungwa,"alisema.

Alitoa wito kwa Watanzania wenye maoni yao kujiandaa kushiriki kwa ukamilifu katika mchakato huo na kutoa maoni ambayo yatawezesha nchi kuwa na Katiba itakayokidhi matakwa ya sasa na ya miaka 50 ijayo.

Tangazo la Rais Kikwete kuhusu kuanza kwa mchakato wa kuandikwa kwa upya kwa Katiba, ni faraja kwa makundi mbalimbali ya kijamii ambayo tangu kumalizika kwa uchaguzi mkuu, Oktoba 31, 2010 yamekuwa yakitoa wito wa kaundikwa kwa Katiba mpya.

Moto wa kudai katiba mpya, uliwashwa na Chadema Novemba mwaka jana, baada ya kutangaza kutotambua kura zilizomweka madarakani Rais Kikwete. Kutokana na hali hiyo, chama hicho kilianza mchakato wa kushikiza kuundwa kwa katiba mpya kwa kususia hotuba ya Rais Kikwete wakati wa akizindua Bunge la Kumi.

Pia wabunge pamoja na viongozi wa chama hicho walisusia sherehe za kuapishwa kwa Rais. Katika kuendeleza madai hayo, hizi karibuni mbunge wa Jimbo la Ubungo kupitia Chadema John Mnyika aliwasilisha hoja binafsi kwenye Ofisi za Bunge, hoja iliyokuwa na lengo la kudai katiba mpya.

Hivi karibuni pia, CUF walifanya maandamano ya kuwasilisha rasimu ya katiba mpya kwa waziri wa Katiba na Sheria. Pia viongozi mbalimbali wastaafu, walipo madarakani wamekuwa wakieleza umuhimu wa kuwa na Katiba mpya.

Miongoni mwa waliojitokeza adharani na kuunga mkono uwepo wa katiba mpya ni pamoja na Rais Mstaafu, Benjamin Mkapa, mawaziri wakuu wa zamani, Joseph Warioba na Frederick Sumaye , Jaji Mkuu Mstaafu na Agostino Ramadhani, Mwanasheria Mkuu wa Zanzibar, Jaji Omar Makungu pamoja na waziri Mkuu, Mizengo Pinda ambaye aliahidi kumshauri Rais juu ya suala la kuundwa kwa Katiba mpya.

Madai ya Katiba mpya pia yamewahi kutolewa na Msajili wa Vyama vya Siasa, John Tendwa ambaye alisema bayana kuwa katiba mpya iandikwe mapema kabla ya mambo kuwa mabaya, akitoa mfano wa mapungufu ya katiba ya sasa kuwa ni rais kupewa madaraka makubwa.

Lakini akiwa Ikulu kwenye hafla ya kuapishwa Jaji Mkuu Mpya, Mohamed Othman Chande, Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG) Frederick Werema, alisema kuwa haona haja ya kuandikwa katiba mpya badala yake katiba iliyopo, iwekewe viraka.

“Kuandika Katiba mpya hapana, lakini kufanya marekebisho kwa kuondoa au kuongeza mambo fulani kwenye katiba, ruksa,” alisema Jaji Werema.

Wakati huohuo, Rais Kikwete ameutangaza mwaka 2011 kuwa mwaka wa maadhsimisho ya miaka 50 ya Uhuru ambayo kilele chake kitakuwa tarehe 9 Desemba, 2011 ambapo kutafanyika sherehe kubwa na za aina yake nchi nzima na wananchi kushirikishwa kikamilifu.

"Kwa kutambua umuhimu wa aina yake wa maadhimisho ya mwaka huu ya siku ya Uhuru wa Tanzania Bara tarehe 9 Desemba, 2011, tumekubaliana na viongozi wenzangu serikalini kuwa tusherehekee siku hiyo kwa uzito unaostahili," alisema.

Kadhalika Rais alisema jambo jingine ni kufanyika kwa tathmini ya kina ya mafanikio tuliyoyapata na tahmini hizo kuandikwa katika vitabu ili kuhifadhi kumbukumbu hizo muhimu kwa vizazi vijavyo.

"Vitabu na nyaraka hizo vitakuwa kumbukumbu zenye manufaa makubwa kwa wenzetu watakaokuwepo mwaka 2061 wakati wa kusherehekea miaka 100 ya Uhuru wa Tanzania Bara" alisema na kuongeza kuwa pia yatafanyika maonyesho maalum katika Uwanja wa Maonyesho wa Julius Nyerere, Dar es Salaam na kote mikoani kwenye viwanja vya maonyesho, kuelezea mafanikio yaliyopatikana katika nyanja mbalimbali katika miaka 50 tangu Uhuru wa Tanzania Bara.
Angalia video................. JK 2011

Wauwa Katika Mkesha wa Mwaka Mpya

Alexandria,Misri
Watu 21 wauwa wakitoka kwenye misa ya mwaka mpya


Abuja,Nigeria
Kumetokea mlipuko mkubwa katika eneo lenye mkusanyiko mkubwa wa watu
Walikuwa wapo kwenye Mkesha wa Mwaka Mpya
Takribani watu 4 wauawa na 13 kujeruhiwa kwa mujibu wa maofisa wa polisi
wakati TV ya Taifa imetoa idadi ya waliouwa ni watu 30.

Friday, December 31, 2010

Kali Za Funga Mwaka

Huko Afrika kusini,kumekuwa na heka heka za mwisho kwa raia wa Zimbabwe kujiandikisha kisheria.
Raia Wazimbabwe atakaye kuwa hajajiandikisha atajikuta anarudishwa nchini Zimbabwe.

Mwezi Aprili ,2009 serikali ya Afrika kusini ilitoa ruhusa kwa Wazimbabwe kuingia nchi hiyo bila kibali kufuatia hali mbaya ya kisiasa na kiuchumi.Kusamehemewa Viza kwa Wazimbabwe,kulikuja kutokana na mazungumzo baina ya nmawaziri wa mambo ya ndani wa Zimbabwe na mwenzake wa Afrika kusini.



Huko Uhispania,wanawake wajawazito wamejikuta wakiharakisha kujifungua ili kuweza kupata posho toka serikalini.
Mabadiliko ya sheria ya mafao ya uzazi yataanza rasmi tarehe mosi 2011,ambapo serikali ya Uhispania imetangaza kusimamisha rasmi utoaji wa posho ya US$ 3000.
Kudidimia uchumi wa Uhispania kumepelekea serikali kusimamisha
posho ya ulezi .

Lengo la utoaji wa posho hiyo,ambayo ilianza rasmi mwaka 2007 lilikuwa ni kuwahamasisha raia wa Uhispania kuongeza vizazi ili kukabiliana tatizo la uhaba wa watu .

"Ili Uhispania kuendelea, inahitaji kuwa familia zenye watoto wengi.Na familia itabidi ihitaji misaada zaidi ili kuweza kuwa na watoto wengi na vyanzo vingi ili kumudu ulezi", Zapatero aliliambia bunge mwaka huo.
Zaidi soma .Aljazeera

Estonia tarehe 1/1/2011 itakuwa mwanachama wa 17 wa muungano wa sarafu wa ulaya,ni nchi ya kwanza toka Muungano wa nchi za soviet kujiunga na umoja wa Ulaya na Nato mwaka 2004.



Brazil -Kwa heri Lula ,karibu Dilma Roussef
Anaanza kazi rasmi tarehe 1/1/2011.
Mwanamke wa kwanza kuwa rais,nchini Brazil

Australia-Sura Tatu Zakaribisha Mwaka Mpya

Kaskazini Ya Australia Yakumbwa na Mafuriko
Ukubwa wa eneo la Kaskazini ni sawa na nchi
ya Ujerumani na Ufaransa kwa pamoja au kwa
nchi kama Marekani ni eneo zima la Texas.
Watu takribani 200000 waokolewa


Kusini Mashariki ya Australia yakubwa na ongezeko kubwa la joto

Hatimaye Mji wa Sydney wafurahia Ujio wa mwaka mpya

Thursday, December 30, 2010

Waziri Akataa Kuuziwa Mkaa Korogwe


Waziri wa Maliasili na Utalii,Ezekiel Maige

Wauza mkaa katika eneo la kijiji cha Chekeleni, wilayani Korogwe mkoani Tanga, walivamia gari la Waziri wa Maliasili na Utalii, Ezekiel Maige, baada ya kusimama ghafla katika eneo hilo na kutaka wamuuzie mkaa wao, wakifikiri ni mteja wa kawaida.


Hata hivyo, ndoto za wafanyabiashara hao ziliyeyuka ghafla, baada ya kubaini kwamba, Waziri Maige si mteja kama walivyofikiria, bali alisimama hapo kutaka kuona kama wanauza mkaa huo kihalali.

Baada ya kugundua kwamba wanayemshawishi anunue mkaa wao ndiye Waziri wa Maliasili na Utalii, wafanyabiashara hao waliokuwa wamepanga maguni ya mkaa pembezoni mwa barabara, waliamua kutimua mbio na kuacha mkaa wao, huku waliobaki katika eneo hilo, wakikana kujihusisha na biashara hiyo.

Waandishi wa habari waliokuwa kwenye msafara wa Waziri Maige, walipata fursa ya kuzungumza na baadhi ya wananchi ambapo walidai kuwa wamekuwa wakiuza mkaa kwa Shilingi 7,500 kwa gunia moja.

Wananchi hao walisema kuwa wamekuwa wakiuza mkaa huo kila siku ili waweze kujipatia ridhiki na kwamba baadhi ya maafisa misitu wamekuwa wakiwaomba chochote (rushwa) ili wawaruhusu kuendesha biashara hiyo ikiwa ni pamoja na kutoa ushuru wa Sh. 1,000.

“Hata hivyo, tunashindwa kuelewa maana mara waje watu wengine na kujiita watu wa TRA, tunawapa ushuru na tunaposhindwa kutoa wanachukua mkaa na kuondoka nao. Mara nyingine wanakuja watu wa halmashauri tunatoa ushuru gunia Sh. 1,000,” alisema mwananchi mmoja na kuoinyesha risiti ya magunia 50.

Mwenyekiti wa kijiji hicho, Athuman Said, alirusha lawama kwa baadhi ya watumishi wa serikali kwamba wao ndio chanzo cha ushuru wa mazao ya misitu kupotea kwa sababu wamekuwa hawatekelezi majukumu yao ipasavyo.

Hata hivyo, mwenyekiti huyo ameishauri serikali kuwabana wachoma mkaa ili waweze kutoa ushuru badala ya kuwabana wafanyabiashara wadogo wadogo tu.

Kwa upande wake, Waziri Maige, aliagiza kwamba maafisa misitu wahakikishe kila anayefanya biashara ya mkaa anatoa ushuru wa Shilingi. 2,000 kwa gunia moja na kwamba wasimamie ipasavyo sheria namba 14 ya mwaka 2004, inayohusu mazao ya misitu.

Waziri Maige aliwataka wananchi kuhakikisha pindi wanaponunua mkaa wapewe risti, ili kuepuka usumbufu unaoweza kujitokeza na kwamba wakikutwa wakiwa hawana risti watakamatwa kwa mjibu wa sheria.

Waziri Maige aliwaambia wananchi hao kuwa kudai risiti kutasaidia kukusanya mapato ya serikali kwa kiwango kinachotakiwa kwani wakwepaji wa ushuru watakuwa wamedhibitiwa.

“Wananchi wahakikishe pindi wanapouziwa mkaa wapewe risti na muuzaji huyo, maana ukikamtwa huna risiti ni kosa. Na hali hiyo itasaidi kuwabana wakwepaji wa ushuru na hivyo kukusanya mapato ya serikali vizuri,” alisema Waziri Maige, ambaye tangu alipoteuliwa kushika wadhifa huo mwezi uliopita, amekuwa akichukua hatua za kubana wizi wa rasilimali za nchi.
Chanzo: Nipashe

Rais Wa Zamani Wa Israel Apatikana Na Hatia Ya Ubakaji


Rais wa zamani wa Israel,Moshe Katsav

Rais wa zamani wa Israel Moshe Katsav amepatikana leo na hatia ya makosa mawili ya ubakaji, ikiwa ni kilele cha kashfa iliyojitokeza miaka minne iliyopita ambayo ililishangaza taifa hilo la Kiyahudi. Rais huyo wa zamani anakabiliwa sasa na hukumu ya kwenda jela miaka minane.


Wakati mahakama hiyo mjini Tel Aviv ikitoa hukumu hiyo, ambapo pia imemhukumu Katsav kwa madai ya bughdha za kingono, vitendo vinavyovuka mipaka na kuzuwia sheria kuchukua mkondo wake, rais huyo wa zamani mwenye umri wa miaka 65 ambaye alionekana dhahiri kufadhaika, alikuwa akinong'ona tu, "hapana , hapana".

Hukumu hiyo inakuja baada ya kuendeshwa kesi hiyo ambayo imechukua mwaka mmoja na nusu na kujumuisha madai ambayo ni ya kuhuzunisha, yakimuonesha Katsav kuwa ni mbakaji ambaye mara kwa mara huwasumbua wafanyakazi wanawake katika ofisi yake.

Kiongozi huyo wa zamani wa nchi anashutumiwa kwa kumbaka mara mbili mwanamke mmoja ambaye ametambuliwa kwa jina la "Aleph" wakati akiwa waziri wa utalii, na kuwafanyia usumbufu kingono na kuwabughudhi wanawake wengine wawili wakati akiwa rais. Katsav amesema kuwa hana hatia wakati wote wa uchunguzi wa kesi hiyo ya ubakaji na usumbufu wa kingono.

Awali alikubali makubaliano ya kutoa maelezo yake mahakamani ambayo yangemfanya kukubali madai madogo madogo na kulipa faini ili waendesha mashtaka watupilie mbali madai ya ubakaji, lakini baadaye alibadili msimamo wake, na kufanya makubaliano hayo kuwa batili na kusema anataka kusafisha jina lake mahakamani.

Alilazimika kujiuzulu kama rais , akakabidhi ofisi kwa hasimu wake Shimon Peres. Katsav amewashutumu wahanga wake kwamba wanajaribu kumwendea kinyume na kudai kuwa alikuwa mhanga wa juhudi za kumchafulia jina zinazofanywa na kundi la waendesha mashtaka na vyombo vya habari bila ya yeye kuweza kujitetea. Mwanawe wa kiume Boaz Katsav, baada ya kutolewa hukumu hiyo amesema kuwa baba yake hana hatia.

Tunataka kukata rifaa. Na kwa msaada wa Mwenyezi Mungu, kila mmoja atatambua kuwa baba yangu , rais wa nane wa taifa la Israel hana hatia.

Waziri mkuu wa Israel, Benjamin Netanyahu amesema kuwa ni siku ya masikitiko kwa taifa la Israel na raia wake, lakini ameisifu kesi hiyo kuwa ni ishara ya nguvu za mfumo wa sheria wa nchi hiyo.
Chanzo: Dw

Wednesday, December 29, 2010

Bei Mpya Za umeme Hizi Hapa

SHIRIKA la Umeme nchini (TANESCO) limeainisha gharama mpya kwa watumiaji wa umeme zitakazoanza kutozwa kuanzia mwezi Januari mwakani.

Taarifa iliyotolewa kwenye vyombo vya habari na Ofisi ya Uhusiano wa Tanessco jijini Dar es Salaam jana ilianisha kuwa gharama hizo mpya zimegawanyika katika makundi matatu kulingana na mahitaji ya matumizi ya umeme.

Makundi hayo ni pamoja na watumiaji wa nishati hiyo kwa matumizi ya majumbani ambapo gharama ya chini kutoka 0-50 kWh/mo utauzwa kwa gharama ya sh 60 badala ya sh 49 ya sasa, tofauti yake ikiwa sh 11.

Kwa upande wa matumizi ya umeme ya kawaida bei ya matumizi kwa gharama za nishati kwa uniti imepanda kutoka sh 129 hadi kufikia Sh 157 ikiwa imeongezeka kwa sh 28.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo, kadhalika kwa upande wa mahitaji ya juu ya msongo mdogo, gharama za nishati kwa uniti imepanda kutoka sh 85 hadi sh 94 ikiwa imepanda kwa sh 9 zaidi.

Kadhalika mahitaji ya juu ya msongo mkubwa, gharama za nishati kwa uniti ambao ulikuwa ukiuzwa sh 79 sasa utauzwa sh 84 tofauti ikiwa ni sh tano.

Kwa upande wa Shirika la Umeme Zanzibar gharama za nishati kwa uniti kwa gharama mpya ya umeme itakuwa ni sh 83 badala ya sh 75 gharama hizo zikiwa zimepanda kwa sh 8.

Watumiaji ambao wameonekana kuumizwa katika gharama hizi mpya ni wale wa matumizi madogo madogo ya nyumbani na wenye matumizi ya kawaida ambao wamepandishiwa kwa zaidi ya Sh 10.

Kwa muhibu wa taarifa za TANESCO, hatua hiyo ya ongezeko la gharama imefikiwa baada ya gharama hizo kuidhinishwa na Mamlaka ya Udhibiti wa Nishati na Maji (EWURA).

Dk. Slaa Aacha Kilio CCM

USHINDI mwembamba wa Chama cha Mapinduzi (CCM) uliosababisha ruzuku yake kuporomoka, umekiweka chama hicho mahali pabaya baada ya watendaji wake kushindwa kulipana mishahara.

Chama hicho tawala kimefikia hatua ya kushindwa kuwalipa watendaji wake hasa wale wa nchini na kupunguza matumizi baada ya ruzuku yake kushuka kutoka zaidi ya sh bilioni moja hadi sh milioni 800,000 baada ya mgombea urais wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Dk. Willbrod Slaa kupunguza kura za Rais Jakaya Kikwete kwa kiwango kikubwa.

Habari kutoka ndani ya makao makuu ya CCM, zinasema chama hicho kimepunguza matumizi yake kwa kiasi kikubwa na mara nyingi Katibu Mkuu wa chama hicho, Yusuf Makamba, amekuwa akiwaambia watendaji hao kwamba hali hiyo inatokana na kupungua kwa ruzuku.

'Sasa hivi hakuna cha vocha wala pesa za posho kama zamani. Tunaambiwa tujitolee, watendaji wa chini waliokuwa wakipelekewa pesa kila mwezi, kama hawawezi kujiendesha, wasitegemee pesa toka makao makuu,' alisema mmoja wa maafisa wa chama hicho, ofisi ndogo ya Lumumba, Dar es Salaam.

Mbali ya kushindwa kulipana mishahara, habari zaidi zinasema watu walioathirika na kimbunga cha Dk. Slaa ni taasisi za CCM ambazo ndizo zilikuwa kinara wa kumpinga Dk. Slaa wakati wa kampeni.

Taasisi hizo zinazomegewa ruzuku kila mwezi mgao wao umepungua na kuna uwezekano wa baadhi yao kufutiwa kabisa.

Baadhi ya taasisi zinazopata ruzuku toka makao makuu ya CCM ni pamoja na kundi la muziki wa dansi, kwaya na maigizo la Tanzania One Theatre (TOT), Radio Uhuru, Kampuni ya Magazeti ya Uhuru na Mzalendo, jumuiya za chama ambazo ni Umoja wa Vijana (UVCCM), Jumuiya ya Wanawake (UWT) na Jumuiya ya Wazee CCM (TAPA).

'Kwanza TOT, magazeti ya Uhuru na Mzalendo na Radio Uhuru, yanaweza kufutiwa kabisa ruzuku maana hakuna maana ya kuwapa ruzuku kama wanapaswa kujiendesha kibiashara na wanapata faida. Mpango huo umeanza kujadiliwa sana pale makao makuu,' alisema mmoja wa makada wa CCM ambaye ni mjumbe wa Halmashauri Kuu.

CCM inapata kiwango sh milioni 800 kutokana na kupata asilimia 60.40 ya kura za urais katika uchaguzi huo, ambazo ni sawa na sh milioni 354 na asilimia 77 ya wabunge (sawa na sh milioni 460) kwa mwezi.

CHADEMA inapata sh milioni 203.6, kwa kupata asilimia 24 ya kura za urais (sawa na sh milioni 146) na asilimia 9.62 ya wabunge (sawa na sh milioni 56) wakati CUF, sasa inapata sh milioni 117.4, kutokana na kupata asilimia 9.80 ya kura za urais (sawa na sh milioni 57.9) na asilimia 10 ya wabunge (sawa na sh milioni 56).

NCCR-Mageuzi inapata ruzuku ya sh milioni 10 kutokana na kupata asilimia 1.08 ya wabunge wakati UDP na TLP vinapata ruzuku ya sh milioni 2.4 kwa kupata asilimia 0.42 ya kura za ubunge kila kimoja.

Kwa mujibu wa sheria ya uchaguzi, ruzuku hiyo hutolewa kwa chama kilichofikisha kuanzia asilimia tano ya kura za urais na kwa uwiano wa wabunge na madiwani, ambao chama kilivuna katika uchaguzi huo.

Ruzuku hiyo ilianza kutolewa Novemba, baada ya Uchaguzi Mkuu uliofanyika nchini Oktoba 31, mwaka huu na ule uliofanyika baadaye katika baadhi ya majimbo kukamilisha uchaguzi huo.

Katika uchaguzi mkuu uliopita, Rais Kikwete alipata ushindi mwembamba wa kura milioni tano, sawa na asilimia 61.17, akifuatiwa na Dk. Slaa aliyepata kura 2,271,941, sawa na asilimia 26.34, wakati mgombea wa CUF Profesa Ibrahim Lipumba aliambulia kura 695,667, sawa na asilimia 8.

Chanzo: Tanzania Daima

Monday, December 27, 2010

Sitta Asubiria Taarifa Rasmi Kuhusu Hoja Ya Mgeja

Vinara wakukemea ufisadi

Waziri wa ushirikiano wa Afrika Mashariki,Spika wa
mstaafu Samuel Sitta akiwa na Mbunge wa SameMashariki
Bi Anna Kilango.

WAZIRI wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Samuel Sitta, amesema amasubiri kwa hamu hoja binafsi iliyoahidiwa kuwasilishwa Halmashauri Kuu ya CCM na Mwenyekiti wa chama hicho Mkoa wa Shinyanga, Hamis Mgeja,.

Alhamisi iliyopita, Mgeja alimtuhumu Sitta kuwa anaendeleza mgawanyiko ndani ya CCM na kumtaka afute kauli yake kuwa aliondolewa uspika kwa mizengwe, la sivyo atawasilisha hoja binafsi Nec kumtaka athibitishe. 
“Sitta anapaswa kufuta kauli yake kuwa, aliondolewa kwa hila…kikao kilichofanya uamuzi kuhusu nafasi ya uspika ni Kamati Kuu ya CCM. Kwa hiyo anamaanisha wajumbe wa kikao hicho wana hila naye.

Kusema hivyo kutasababisha baadhi ya wanachama kukosa imani na kikao hicho,” alisema Mgeja. 
Akizungumza na gazeti hili juzi, Sitta alisema ingawa hajapata taarifa rasmi kuhusu hoja za Mgeja, anaisubiri kwa hamu.

“Siwezi kuzungumzia kwa kina taarifa ya Mgeja kwa kuwa sijaipata vizuri, lakini ninaisubiri kwa hamu hoja yake hiyo,’’ alisema Sitta ambaye alikuwa Spika wa Bunge la Tisa.

Wakati Sitta akisita kujibu hoja ya Mgeja, Mbunge wa Same Mashariki (CCM), Anne Kilango, amemshangaa Mwenyekiti huyo wa CCM Mkoa wa Shinyanga, akisema alichosema hakiwezekani.
Pia, Kilango alipuuza msimamo wa Mgeja akisema hauna mashiko: "Hoja binafsi zinapelekwa bungeni tu, sio kwenye vikao vya chama. Vikaoni zinaletwa ajenda, sasa huoni haya ni maajabu?"

“Huyu mwenyekiti asituvuruge, tunatakiwa kujua chama kinaelekea wapi na tumefikaje hapa,” alisema Kilango na kueleza kuwa anaamini Mgeja katumwa, huku akiongeza:

"Ni bora pia atwambie (Mgeja) ametumwa na nani kwa kuwa anachozungumza ni kudanganya umma."

Kilango ambaye alikuwa akizungumza kwenye mahojiano maalumu na gazeti hili nyumbani kwake jijini Dar es Salaam jana, alisema anamshangaa mwenyekiti huyo kumwandama Sitta, badala ya kutafakari jinsi alivyopoteza majimbo manne ya ubunge mkoani Shinyanga.

"Huyu anataka tumkate panya mkia halafu aendelee kuishi badala ya kumkata kichwa ili kumaliza tatizo," alisema Kilango akimaanisha kuwa Mgeja anataka kukwepa hoja ya msingi kwa kuanza kuzungumzia mambo yasiyomhusu.

"Namsihi Mwenyekiti wa CCM Taifa, Rais Jakaya Kikwete, asikubali kuwa na viongozi ndani ya chama ambao wanataka kumkata panya mkia badala ya kumkata shingo ili afe," alisema Kilango.

Alisema hivi sasa CCM inatakiwa kuokoa chama kwa kufanya tathmini kujua chanzo cha wananchi kuwakataa, lakini sio kuzungumzia mambo yasiyo na msingi.

Desemba 19, mwaka huu, Sitta alitoa kauli nyingine inayoweza kutikisa CCM baada ya kueleza kuwa, aliondolewa kwenye kinyang'anyiro cha Spika wa Bunge kutokana na hila za viongozi, ambao walishindwa kuhimili kasi ya utendaji wake kwenye chombo cha kutunga sheria.

Mbunge huyo wa Urambo Mashariki, alijikuta akianguka kwenye kinyang'anyiro hicho baada ya CCM kwa kile kilichoelezwa kuwapa wanawake nafasi ya kuongoza moja ya mihimili ya nchi.
Chanzo: Mwananchi.

Sunday, December 26, 2010

JK AMTEUA MOHAMED CHANDE OTHMAN KUWA JAJI MKUU MPYA

                                                                                                      

                                    UNITED REPUBLIC OF TANZANIA
                      DIRECTORATE OF PRESIDENTIAL COMMUNICATIONS
                                  Telephone: 255-22-2114512, 2116539
                                       E-mail: press@ikulu.go.tz
                                  Website: www.mawasilianoikulu.go.tz
                                       Fax: 255-22-2113425


                                       PRESIDENT’S OFFICE,
                                       THE STATE HOUSE,
                                        P.O. BOX 9120,
                                        DAR ES SALAAM.
                                        Tanzania.


                           TAARIFA YA IKULU
Rais Jakaya Mrisho Kikwete, amemteua Jaji Mohamed Chande Othman kuwa Jaji Mkuu wa Tanzania, kuanzia tarehe 28 Disemba, 2010.

Jaji Othman anachukua nafasi ya Jaji Augustino Ramadhani anayestaafu kwa mujibu wa sheria tarehe 27 Disemba, 2010.

Jaji Othman amekuwa Jaji wa Mahakama Kuu na Mahakama ya Rufaa kwa muda miaka saba(7).

Kwa sasa Jaji Othman ni Jaji wa Mahakama ya Rufaa na pia ni mtaalamu binafsi juu ya hali ya Haki za Binadamu huko Kusini mwa Sudan, hadi mwezi Agosti 2011.

Jaji Othman alizaliwa tarehe 1 Januari, 1952, ana shahada ya kwanza ya Sheria (LLB) ya Chuo Kikuu cha Dar-Es-Salaam na Shahada ya Uzamili (MA) kutoka katika Chuo Kikuu cha Webster, Geneva-Uswisi.

Amewahi kuwa Makamu wa Mwendesha Mashtaka wa Mahakama ya Rwanda huko Arusha na amewahi kushika nafasi sawa na Mwanasheria Mkuu wa Serikali huko Timor Mashariki.

Jaji Othman pia, amewahi kufanya kazi ndani na nje ya nchi katika Mashirika mbalimbali ya Kitaifa na Kimataifa kama vile Mpango wa Maendeleo wa Umoja wa Mataifa (UNDP) na Shirika la Msalaba Mwekundu.

Jaji Othman ataapishwa kesho tarehe 27 Disemba, 2010 katika viwanja vya Ikulu saa 4:00 asubuhi.

                                      Michael P. Mwanda,
                                      Kaimu Katibu Mkuu Kiongozi,
                                                 Ikulu.
                                          DAR ES SALAAM.
                                          26 Disemba, 2010
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...